ATIMAYE Donald Trump, Rais wa Marekani amevaa barakoa hadharani tangu janga la corona (COVID-19) liteke Marekani. Inaripoti mitandao ya kimataifa…(endelea).
Trump ameonekana akiwa na barakoa wakati alipotembelea Hospitali ya Kijeshi ya Walter Reed iliyopo nje ya Jiji la Washington.
Kiongozi huyo wa Marekani, ambaye alikwenda kukutana na wanajeshi waliojeruhiwa pia wahudumu wa afya.
“Sijawahi kamwe kupinga uvaaji wa barakoa, lakini ninaamini kuwa zina mahali na muda wake,” amesema alipokuwa akiondoka katika Ikulu ya White House.
Awali, alisema kuwa hawezi kuvaa barakoa na akamkejeli hasimu wake wa chama cha Democrat, Joe Biden kwa kufanya hivyo.
“Ninafikiri pale unapokua hospitali, hasa katika hali fulani, ambapo unaongea na wanajeshi na watu, ambao wakati fulani wametoka kwenye meza za upasuaji, nafikiri ni kitu kizuri kuvaa barakoa,” amesema.
Akizungumza na kituo cha habari za biashara cha – Fox Business Network wiki iliyopita, Trump alisema “ninaunga mkono barakoa.”
Aliongeza kuwa “ni kama ninapenda ” anavyofanana akiwa ameivaa, akijifananisha na aliyovaa Lone Ranger, shujaa wa kufikirika ambaye pamoja na rafiki yake mzawa wa Marekani, Toronto, walipigana na wahalifu katika Marekani ya zamani ya Magharibi.
Wakati vituo vya Marekani vya udhibiti wa magonjwa (CDC) Aprili vilipopendekeza kuwa watu wavae barakoa au vitambaa vinavyofunika midomo na pua wawapo katika maeneo ya umma ili kusaidia kuzuwia kusambaa kwa virusi, Trump aliwaambia waandishi wa habari kuwa hatafuata agizo hilo.
“Sidhani nitakua nikifanya hilo” alisema wakati huo na kuongeza “kuvaa barakoa huku nikiwasalimia marais, mawaziri wakuu, madikteta, wafalme na mamalkia – sioni hili likifanyika.”
Baadhi ya taarifa za vyombo vya habari zimesema, washirika wake wamekua wakimuomba mara kwa mara avae barakoa awapo hadharani.
Leave a comment