UONGOZI wa klabu ya Coastal Union umekanusha taarifa za kuwa imeachana na kocha wake, Juma Mgunda baada ya matokeo mabovu ya hivi karibuni. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa hii leo tarehe 4 Mei 2021 na kudai taarifa hiyo haina ukweli.
Katika taarifa hiyo uongozi wa klabu hiyo umewataka mashabiki na wanachama wao kupuuza taarifa hiyo na kwamba Mgunda bado ataendelea kukinoa kikosi hiko chenye maskani yake mkoani Tanga.
Mgunda ambaye pia ni kocha msaidizi wa kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ ameiongoza Coastal Union kwenye michezo 28 ya Ligi Kuu Tanzania Bara mpaka sasa.
Katika michezo hiyo Mgunda amefanikiwa kushinda michezo nane, kwenda sare tisa na kupoteza michezo 11, safu yake ya ushambuliaji imefanikiwa kupachika mabao 19 na kuruhusu kufungwa mabao 38 na kushika nafasi ya 10 kwenye msimamo akiwa na pointi 33.
Leave a comment