KATIBU Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania- Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo amewaagiza wabunge wote wa Bunge wa chama hicho, kurejea kwenye majimbo yao ili kusikiliza changamoto na kuzitafutia ufumbuzi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Rukwa…(endelea).
Chongolo ametoa maagizo hayo jana Jumatano, tarehe 7 Julai 2021, katika kikao cha ndani cha viongozi mbalimbali wa chama na Serikali katika siku ya kwanza ya ziara ya Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya CCM, katika mji mdogo wa Laela, Sumbawanga Vijijini, Mkoa wa Rukwa.
“Nawapongeza wabunge niliowakuta kwenye mikoa yao baada ya Bunge la bajeti kumalizika, sasa kazi yenu wabunge ni kupita kwenye jimbo lote kuwaeleza wananchi yaliyopitishwa kwenye bajeti, yanayowagusa,” amesema
Katibu mkuu huyo amewataka, wabunge kaeni kwanza na madiwani wawasikilize ndipo wapange ratiba ya ziara zao kwendakwa wananchi.
Alisema, baada ya wabunge kulalamika kuhusu ubovu wa barabara, Rais Samia Suluhu Hassan, alisikiliza kilio cha wabunge hao na kuamua kutoa Sh.500 milioni kwa kila jimbo ili kuzihudumia.
Barabara hizo, zinawahudumia Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (Tarura) ambazo, Rais Samia amesema, anakusudia kuziboresha kifedha na kitaaluma ili kuhakikisha barabara zote nchini zinapitika nyakati zote.
“Natoa maagizo kwa wabunge wote nchini ambao ni zao la CCM kwa sasa wamemaliza Bunge la bajeti, wabunge wote waende kwenye majimbo yao wakawaeleze wananchi yaliyomo kwenye bajeti na hususani yanayowagusa ili waelewe nini serikali inataka kufanya kwao,” alisema Chongolo
Aidha, Chongolo aliwataka viongozi wa CCM ngazi za mikoa, wilaya na kata kwenda kwenye mashina na matawi kufanya mikutano ya kuwasikiliza na kutoa muongozo wa chama hicho katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku ili kubaini changamoto na kuzishughulikia kwa wakati.
Leave a comment