KATIBU mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa Daniel Chongolo amesema ipo haja ya Waziri wa Kilimo Hussein Bashe kutembelea na kutatua mgogoro wa mradi wa umwagiliaji wa Luhindo wenye thamani ya sh mil 900.1 ambao licha ya kukamilika miaka mitatu iliyopita bado haijaanza kufanya kazi. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Chongolo alisema hayo akiwa Wilayani Mvomero mkoani hapa kwenye ziara yake ya siku 9 ambapo alisema haiwezekani Serikali ikatoa fedha nyingi katika kukamilisha miradi ya maendeleo kwa ajili ya maendeleo ya wananchi huku bado mradi usifanye kazi na kuondoa maana aliyoitaka Rais Samia Suluhu Hassan ya kuleta maendeleo nchini.
Aidha amewataka viongozi wote wa serikali kuanzia ngazi ya vijiji kuzingatia miiko ya uongozi ili kukabiliana na migogoro ya ardhi inayoendelea kuchipua katika baadhi ya maeneo nchini.
Akizungumzia changamoto ya umeme wa Wakala wa nishati vijijini ( REA) kwa vijiji 60 aliagiza mkandarasi kampuni ya HNXJDL INT Contructirs kuhakikisha wanafika angalau asilimia 80 ya ujenzi ifikapo mwezi Februali mwaka huu au kukamilisha ujenzi huo vinginevyo atasimamishwa kuendelea na ujenzi huo kupisha wakandarasi wengine.
Hata hivyo alimuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero Dk. Philiphine Titus kutengeneza mpango mkakati utakaoonesha gharama halisi za ujenzi na umuhimu ili kuona haja ya kuanza ujenzi wa soko la Mpunga katika Wilaya hiyo.
Awali Mbunge wa jimbo la Mvomero Jonas Van Zeeland alimshkuru Rais Samia kwa kuwasaidia katika kutatua changamoto mbalimbali kwenye wilaya hiyo licha ya kuwepo kwa changamoto kadhaa zinazowakabili wananchi wa Wilaya hiyo.
Alizitaja changamoto zinazowakabili eneo la Dakawa ni pamoja na upatikanaji wa maji ya Bomba, kukamilika kwa Zahanati ya Kijiji na migogoro ya mipaka baina ya vijiji na vijiji
Akiwa katika shina namba 18 kwenye Kijiji hicho akipokea jumla ya wanachama 13 wapya waliojiunga CCM.
Leave a comment