KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo ameomba vitabu vilivyoandikwa na chama hicho kuelezea itikadi zake na matendo ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, vitumike katika mfumo wa elimu nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Pwani … (endelea).
Chongolo ametoa ombi hilo leo Jumamosi, katika mdahalo wa kitaifa wa kuadhimisha miaka 100 ya kuzaliwa kwa Hayati Mwalimu Nyerere, Pwani mkoani Kibaha.
Katibu Mkuu huyo wa CCM, ametaja vitabu hivyo ambavyo vimezinduliwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ikiwa ni, Kitabu cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Chemchem ya Fikra za Kimapinduzi, ambacho ni mkusanyiko wa makala, hotuba, mashairi na tenzi teule za Mwalimu Nyerere.
Kitabu cha pili kinaitwa, Misingi ya Falsafa, Itikadi na Sera za Chama Cha Mapinduzi, ambacho ni matokeo ya uteuzi na uchambuzi wa nyaraka zenye nadharia ya falsafa, itikadi na sera za CCM.
“Kwa ubora wake hatuna shaka vitakidhi masharti na vigezo vya mahitaji ndani na nje ya nchi. Tunaamini wataalamu wetu watavikubali kuwa na hadhi ya kuwa vitabu vya kiada na ziada, katika ngazi mbaliumbali za mfumo wetu wa elimu nchini,” amesema Chongolo.
Chongolo amesema, vitabu hivyo vitasaidia jamii kufanya tafakuri tunduizi kuhusu uongozi na fikra na matendo ya Mwalimu Nyerere, katika nafasi zote alizokuwa nazo kwenye nchi, Afrika na duniani.
“Kwa uhakika vitabu hivi vinatupitisha katika sehemu kubwa ya historia ya maisha ya Mwalimu Nyerere, katika dhana mbalimbali za maendeleo ya Tanzania, Afrika na dunia, ikiwemo uchumi, maendeleo ya sayansi na teknolojia, mahusiano yetu ya ndani na nje ya nchi yetu,” amesema Chongolo na kuongeza:
“Vinatukumbusha wajibu wetu kama taifa katika siasa, kutokea enzi zake hadi sasa ambapo wewe ndiyo Rais. Vinaangazia misingi ya siasa za CCM, itikadi na historia na itikadi ya ujamaa na kujitegemea, ambayo imekuwa imani kuu ya chama chetu.”
Mbali uzinduzi wa vitabu hivyo, Rais Samia amezindua kitabu kingine cha wasifu wa Mwalimu Nyerere, kilichoandikwa na wanazuoni.
Leave a comment