KATIBU mkuu wa chama cha mapinduzi Daniel Chongolo ameiagiza bodi ya maji bonde la wami Ruvu kuongeza kasi katika usimamizi wa rasilimali za maji kwa kupanda miti katika maeneo ambayo yameshaanza kuharibiwa na shughuli za kibinadamu. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Chongolo alisema hayo mjini Morogoro baada ya kuzindua vitalu vya miche ya miti ya aina zaidi ya 10 vilivyoandaliwa na Bonde la maji Wami Ruvu ana maeneo yote ya pembezoni mwa mito ndani ya bonde hilo.
Alisema kupanda miti pembezoni mwa vyanzo vya maji kutasaidia kuzuia mmomonyoko wa udongo na kufanya mto kutokuwa hatarishi kwa wakazi wa mita 1000 kutoka kilipo chanzo Cha maji.
Aidha aliwataka bonde kutoa elimu kwa jamii inayoishi hata mita 1000 toka kilipo chanzo cha maji kujenga tabia ya kupanda miti itakayozuia mmomonyoko wa udongo na hivyo kujikuta wakiishi mahali salama.
Hata hivyo alilipongeza bonde kwa kuandaa shamba la vitalu vya miche ya miti ya kuhifadhi mazingira na kutunza vyanzo vya maji ambapo aliwashauri kuwa na miti mingi zaidi ili watu binafsi na taasisi waweze kuipata na kupanda katika maeneo yao.
Hivyo aliutaka uongozi wa bonde la maji Wami Ruvu kusimamia uundwaji vikundi vya watunzaji mazingira ili kuendelea shughuli za uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji.
Alisema uharibifu wa mazingira ni mkubwa sana na kufanya kuwa na vipindi vy maji mengi kwa muda mfupi na upungufu wa maji na ongezeko la wastani kwa muda mchache.
Hivyo Chongolo aliitaka jamii kubeba jambo la uhifadhi mazingira kama ajenda na sehemu ya maisha yao.
Awali Mkurugenzi wa Bonde la maji Wami Ruvu Elibariki Mmasi alisema Bonde Wami Ruvu linaendelea kuhifadhi mazingira kwa kupanda miti pembezoni mwa mito huku likijiandaa kutangaza mto Ruvu kuwa eneo oevu.
Leave a comment