MWANASHERIA Mkuu mstaafu wa Tanzania(AG), Andrew Chenge, amesema mapendekezo ya mfumo na muundo uliopendekezwa kwenye rasimu ya Katiba mpya kupata wajumbe wa Tume Huru ya Uchaguzi ndio utaondoa kama sio kupunguza malalamiko ya wadau kuhusu tume hiyo. Anaripoti Seleman Msuya, Dar es Salaam…(endelea).
Aidha Mbunge huyo mstaafu wa Bariadi mkoani Simiyu amesema Katiba mpya kwake sio kipaumbele, huku akisitiza maridhiano kama moja ya nguzo muhimu ya kuendesha nchi.
Chenge ametoa ushauri huo leo Ijumaa tarehe 15 Julai, 2022, baada ya kutoka kutoa maoni kwenye Kikosi Kazi cha Rais Samia Suluhu Hassan cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa.
Amesema rasimu ya Katiba mpya iliyopendekezwa na Tume iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba, iliweke mfumo mzuri wa kupata wajumbe wa Tume ya Huru ya Uchaguzi kuwa wapatikane kwa kuomba nafasi husika.
Amesema eneo hilo ameliishi wakati anahuduma kama mwanasheria Mkuu wa Serikali, hivyo anatambua changamoto zilizopo.
“Eneo la Tume Huru nimekishauri Kikosi Kazi kichukue mapendekezo yaliyopo kwenye rasimu ya Katiba mpya ambayo inataka wajumbe wapatikane kwa kuomba.
Huwezi kuingiza wanasiasa katika tume halafu utarajie kuona usawa, lakini pia huwezi kumkwepa Rais kwenye uteuzi kinachohitajika ni wahusika waombe wafanyiwe usahili na wale wenye sifa ndio wateuliwe,” amesema.
Amesema iwapo waombaji watakuwa na sifa ambazo zimetajwa na rasimu na Kamati ya mchujo ikipitia kwa kina hakutakuwa na lawama za wanasiasa kuingia.
Kuhusu hitaji la Katiba mpya kama inavyodaiwa kihitajika amesema haoni sababu ya kukimbilia huko, bali jamii ijikite kwenye maridhiano.
Chenge amesema Rais Samia ameanza vizuri kwa kusimamia maridhiano hivyo kuitaka jamii imuunge mkono.
Leave a comment