CHELSEA imeshinda kombe la klabu bingwa duniani jana tarehe 12 Februari, 2022 baada ya kuibuka na ushindi wa bao 2-1 dhidi ya Palmeiras katika fainali iliyopigwa jijini Abu Dhabi katika Ufalme wa Kiarabu. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
‘The Blues’ walihitaji muda wa ziada kushinda taji hilo kwa mara ya kwanza baada ya mechi hiyo kuishia sare ya 1-1 katika muda wa kawaida wa dakika 90.
Mshambuliaji Romelu Lukaku aliipa Chelsea uongozi katika dakika ya 54 kwa bao la kichwa huku Raphael Veiga akisawazishia mabingwa hao wa Amerika Kusini kwa mkwaju wa penalti katika dakika ya 64.
Mechi hiyo iliishia sare ya 1-1 na kulazimisha muda wa ziada ambapo Mjerumani Kai Havertz alifunga penalti katika dakika ya 117 baada ya maamuzi ya refa msaidizi wa video (VAR).
Havertz vilevile ndiye aliyefunga bao la pekee na la ushindi katika fainali ya klabu bingwa Ulaya mwaka jana dhidi ya Manchester City na kuwahakikisha nafasi katika mashindano ya klabu bingwa duniani.
“Inapendeza. Baada ya kuwa mabingwa wa Ulaya, sasa sisi ni mabingwa wa dunia. Inapendeza sana,” Havertz alisema katika mahojiano baada ya mechi hiyo.
Chelsea walilipiza kisasi kwa kupoteza fainali ya kombe hilo mwaka 2012 dhidi ya Corinthians ya Brazil na sasa wameshinda kila kombe tangu klabu hiyo kununuliwa na bwenyeye Roman Abramovich mwaka 2013.
Matajiri hao wa darajani wanakuwa klabu tatu ya Uingereza kufanua hivyo baada ya Manchester United na Liverpool.
Kocha wa Chelsea, Thomas Tuchel alirejea uwanjani baada ya kupona Corona na kusafirishwa hadi Abu Dhabi juzi Ijumaa huku kipa Edouard Mendy akirejea uwanjani baada ya kurejea kutoka mashindano ya mataifa ya Afrika (AFCON) ambako alitawazwa bingwa na timu yake ya taifa ya Senegal.
Leave a comment