CHAMA cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), kimesema muarobaini wa dosari zilizojitokeza katika mchakato wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa, ni Tume Huru na Katiba Mpya. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Hayo amesema Hashim Rungwe, Mwenyekiti wa CHAUMMA Taifa, leo tarehe 11 Novemba 2019 wakati akifanya mahojiano na MwanaHALISI ONLINE.
“Tuachiwe tufanye katiba mpya ya nchi tuondokane na mambo ya huyu mwenyekiti wa tume, hawa wote wanafuata amri ya serikali. Kwa sababu wanalipwa na serikali, lazima wawe na upendeleo, ili wananchi wawe radhi, wafanye tume huru ya uchaguzi,” ameeleza Rungwe na kuongeza;
“Sisi tunataka tume huru ya uchaguzi ambayo sisi sote tutaenda kuilalamikia, sasa hivi sisi tutamlalamikia nani? Kama wanafanya vitu kinyume na sheria, haya mambo yanatia uchungu kwa nini wanatufanyia hivi, kama wao wameinunua nchi, wameinunua kwa bei gani?”
Rungwe amesema CHAUMMA hakitashiriki uchaguzi huo, hadi Tume Huru ya Uchaguzi.
“Mtazamo wa CHAUMMA ni kama tulivyoeleza, kwamba hakiungi mkono kuendelea na uchaguzi sababu tangu mwanzo umeonekana ni batili. CCM wamehodhi uchaguzi na watumishi wamekuwa upande wao. Umejawa ghiliba, haturudi kwenye uchaguzi hadi tume huru ipatikane, tume iliyopo ibadilishwe,” amesema Rungwe.
Leave a comment