SERIKALI ya Tanzania, imesema chanjo ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (Covid-19), imeshaingia nchini. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo Jumatano, tarehe 21 Julai 2021 na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akizungumza katika swala ya Eid El-Adha, iliyofanyika kwenye Msikiti wa Mtoro, Kariakoo jijini Dar es Salaam.
“Chanjo ipo anayetaka akanchanje hospitalini, zimeelezwa mahali zilipo nenda ili utimize haja yako lakini pia ni kinga, wenzetu wanachanja kama kinga,” amesema Waziri Majaliwa.
Waziri mkuu huyo wa Tanzania, amesema chanjo hiyo imeingizwa baada ya watalaamu wa afya kuzifanyia uchambuzi na kubaini kwamba hazina madhara.
“Madaktari wawaliagizwa wafanye utafiti wa chanjo nzuri ambazo watu wametumia hawajapata madhara, tukawaambia fanyeni uchunguzi katika chanjo zote duniani. Kwetu tumepata chache, aina mbili tatu tukasema tuzilete nchini, anayetaka achanje,” amesema Waziri Majaliwa.
Amesema Serikali imeamua kuingiza chanjo hizo, ili kuwaondolea usumbufu wananchi hasa wanaofanya shughuli zao nje ya nchi.
“Serikali ilikaa chini na kutafakari na kugundua kuwa Watanzania wengi ambao wanashughuli mbalimbali, ikiwemo wanaotaka kwenda hija yenye masharti ya kwenda ukiwa umechanjwa na kuna Watanzania wanafanyabiashara nje ya nchi wanataka watu wawe wamechanjwa,” amesema Waziri Majaliwa.
Waziri Majaliwa ameongeza “Rais Samia Suluhu Hassan, akasema hebu tukae pamoja tutafakari hili jambo hao Watanzania wanaotaka kwenda kwenye maeno haya watatimizaje masharti hayo, maamuzi yakafikiwa walete chanjo kadhaa,” amesema Waziri Majaliwa.
Waziri Majsliwa amewataka Watanzania wazidi kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya Covid-19, akisema kuwa nchi ina wagonjwa kadhaa wa ugonjwa huo.
Amewataka Watanzania kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima, kuvaa barako pamoja na kunawa mara kwa mara kwa maji tiririka na sabuni.
Leave a comment