KIUNGO wa klabu ya Simba Clatous Chama amechaguliwa kuwa mchezaji bora wa mwezi Aprili 2021 kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara huku kocha wa kikosi hiko Didie Gomes akishinda tuzo ya kocha bora mwezi huo huo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Wawili hao wamechaguliwa na kamati maalumu ya tuzo ya Ligi Kuu Tanzania Bara mara baada ya kufanya uchambuzi.
Chama ameshinda tuzo hiyo mara baada ya kuwashinda mshambuliaji wa klabu ya Azam fc Prince Dube na kiungo wa Mbeya City Raphael Daud, huku Gomes akiwagalagaza Zuber Katwila anayekinoa kikosi cha Ihefu na Mathias Lulle wa Mbeya City.
Kocha huyo wa Simba amefanikiwa kuingoza Simba kushinda michezo yote mitano ndani ya mwezi huo na kukusanya jumla ya pointi 15 na kupanda kutoka nafasi ya pili hadi ya kwanza kwenye msimamo wa Ligi.
Simba alianza kupata ushindi wa bao 1-0, dhidi ya Mwadui Fc baadae kuibuka na ushindi wa mabao 2-0, dhidi ya Kagera Sugar na kisha kwenda kuchukua pointi tatu dhidi ya Gwambina kwa ushindi wa bao 1-0.
Mara baada ya hapo Simba ikalejea nyumbani na kupata ushindi mnono wa mabao 5-0, dhidi ya Mtibwa Sugar na kisha kuufunga mwezi Aprili kwa ushindi wa mabao 3-1 walipowaalika Dodoma Jiji.
Kwa upande wa Chama ameshinda tuzo hiyo mara baada ya kuhusika katika mabao sita.
Katika michezo hiyo ya mwezi Aprili Chama amefunga mabao mawili na kutoa pasi za mwisho (assist) nne.
Leave a comment