MWANASHERIA Mkuu wa Serikali, Eliezer Feleshi, amesema mwaka huu wataanzisha chama cha mawakili wa umma Tanzania (public bar association) ili kukuza kiwango na stadi za kazi kwa wanasheria wa sekta zote. Anaripoti Apaikunda Mosha TUDARCo…(endelea).
Hayo amezungumza leo Jumatano ya tarehe 21, September 2022, bungeni akizungumzia uchambuzi na maazimio ambayo yametolewa na kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria.
Ameanisha kuwa kuna jumla ya wanasheria 2,550 ambao ni pamoja na waliopo katika halmashauri, na sasa wanaendelea na usajili wa wanasheria wote walio kwenye huduma ya umma.
Amesema kwamba serikali imeona bado kuna haja ya kuhakikisha kwamba sheria ambazo zimetungwa na kwa mujibu wa katiba na sheria za nchi zinakidhi malengo na matakwa ambayo kwayo zimetungwa kutokana na ushahidi ambao kamati imekutana nao wakati wa uchambuzi.
“Katika sheria mama zilizopo takribani 446 na ndogo zaidi ya elfu 40 dosari ambazo zimejitokeza zinaendelea kupungua kadri hatua mbalimbali zinavyochukuliwa,” amesema Felishi.
Amesema Serikali kupitia ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali, inakamilisha muongozo ambao utatumika kuongoza mamlaka ambazo zinatunga sheria ndogo ikiwemo ngazi ya halmashauri, wizara na mamlaka zingine na kwa wote walio na dhamana.
Ameongeza upo umuhimu wa kutoa elimu na kufanya tafiti kwa wote walio na dhamana ya kutunga sheria ndogo kwani sheria mama mchakato wake unahusisha tafiti na mawasilisho katika hatua mbalimbali tofauti na sheria ndogo.
Leave a comment