KAMATI Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), imeteua makatibu wa kanda sita kati ya kanda 10 za chama hicho. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 22 Februari 2020 na Tumaini Makene, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano Chadema, uteuzi huo ulifanyika hivi karibuni katika kikao cha kamati hiyo, kilichoketi jijini Dar es Salaam, chini ya Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa chama hicho.
Makatibu walioteuliwa ni Amani Golugwa, aliyeteuliwa kuwa Katibu Kanda ya Kaskazini, General Reuben Kaduma ( Kanda ya Kusini), Ali Hemedi Mngwali (Kanda ya Pwani), Emmanuel Masonga (Kanda ya Nyasa), Gwamaka Mbughi (Kanda ya Kati), na Kangeta Ismail Kangeta (Kanda ya Magharibi).
Taarifa hiyo imesema uteuzi wa kanda nne zilizobakia ambazo ni, Serengeti, Pemba, Unguja na Victoria, utafanywa na Kamati Kuu hapo baadae.
“Waliokuwa makatibu wa kanda waliomaliza muda wao na hawajateuliwa katika nafasi hizo, wanapangiwa majukumu mengine katika utumishi wa chama,” inaeleza taarifa ya Makene.
Leave a comment