CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema kitaendelea kupigania upatikanaji wa Serikali ya Majimbo, ili kushusha mamlaka kwa wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa Jana na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, katika ziara ya chama hicho barani Ulaya, iliyolenga kuwasilisha wito wake kuungwa mkono kwenye upatikanaji wa katiba mpya,tume huru ya uchaguzi na mazingira mazuri ya ufanyaji siasa nchini.
Akizungumza katika mkutano wa ujumbe wa Chadema na Naibu Waziri Mkuu wa Serikali ya Jimbo la Brandenburg, nchini Ujerumani, Michael Stibgen, Mnyika alisema chama chake kitaendelea kuamini na kupigania sera ya majimbo kama mkakati wa kushusha mamlaka kwa wananchi Kwa ajili ya kuharakisha maendeleo.
“Tumekuwa tukiinadi sera ya majimbo tangu 2005 na katika mchakato wa kupatikana katiba mpya Tanzania tunataka tushawishi wananchi kutuunga mkono na kuingizwa rasmi kwenye katiba,” alisema Mnyika na kuongeza:
“Uwepo wetu nchini Ujerumani ni pamoja na kujifunza mfumo huu wa Serikali za majimbo Ili kuendelea kuboresha sera yetu na kupunguza changamoto katika utekelezaji wake na tumechagua Jimbo la Brandenburg kuwa miongoni mwa mahala pa kupata uzoefu.”
Naye kiongozi wa Ujumbe wa Chadema katika ziara hiyo, Tundu Lissu, ambaye pia Makamu Mwenyekiti Bara, aliipongeza Ujerumani Kwa kuwa na mfumo madhubuti wa majimbo na kuahidi chama chake kitaendelea kujifunza kutoka kwao.
Kwa upande wake Stubgen, aliunga mkono hoja ya Chadema kuhusu upatikanaji wa Serikali za Majimbo, akisema itasaidia uendeshaji wa Tanzania Kwa kuwa ni nchi kubwa.
Alisema mfumo huo una changamoto pia kwa kiasi fulani hasa katika eneo la madilahi ya Serikali Kuu na za majimbo lakini zinatibiwa na uwepo wa Katiba za Serikali Kuu na za Majimbo ambazo zinaelekeza kila jambo namna ya kuzingaitiwa.
“Tuna Katiba ya Serikali Kuu(Federal) na za Serikali za Majimbo (Regional) zinaelekeza masuala mbalimbali ikiwemo ya mapato ,namna ya kupitisha sheria na kanuni jambo ambalo linatoa wepesi katika uendeshaji,” alisema
Leave a comment