CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimetangaza nia ya kukiondoa madarakani Chama Cha Mapinduzi (CCM), ifikapo 2025 kupitia Uchaguzi Mkuu. Anaripoti Mwandishi Wetu. Geita … (endelea).
Ahadi hiyo ilitolewa jana tarehe 27 Desemba 2022 na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika, akizungumza na wanachama wa Chadema, Jimbo la Geita Vijijini, huku akisema kwamba chama chake ni tumaini la Watanzania katika kuwaletea uhuru, maendeleo na demokrasia.
“Tunadhamira ya kuchukua dola na kuongoza nchi 2025, kwa sababu ya dhamira kuu ya kuiondoa CCM na kuongoza Serikali. Hatuwezi kuliacha jimbo lolote nyuma lazima majimbo yote tusonge kwa nguvu kila mahali. Ujumbe wangu huu sio kwa Kanda ya Victoria bali ni kwa kanda zote za Tanganyika na Zanzibar,”alisema Mnyika.
Aidha, Mnyika alisema 2023 utakuwa ni mwaka wa marekebisho ya katiba mpya na upatikanaji tume huru ya uchaguzi, ambayo yameshindwa kufanyika 2022.
“2022 ungekuwa mwaka wa marekebisho lakini hayajakamilika, tukiwaachia 2023 kukapita kama taifa tunakwenda kwenye hatari ya mbele ya 2024 na 2025. Kwa hiyo jambo la kwanza kubwa kwa 2023 unapaswa uwe mwaka wa kuhakikisha tunadai kwa nguvu katiba mpya na tume huru ya uchaguzi,” alisema Mnyika na kuongeza:
“Huwa nawaambia viongozi wenzangu badala ya kusubiri 2024 na 2025 kukawa hakuna tume huru ya kusimamia uchaguzi kutakuwa na nguvu ya kuzuia uchaguzi. Nguvu hiyo itakayotumika 2024 na 2025 tuitumie 2023 kudai katiba mpya na tume huru ya uchaguzi, hili linapswa kuwa jambo kuu la kwanza la taifa.”
Leave a comment