JOHN Mrema, Mkurugenzi wa Mawasiliano, Itikadi, Uenezi na Mambo ya Nje wa Chadema, ameitaka Serikali kutoa kanuni mapema na kutangaza tarehe ya uchaguzi wa serikali za mitaa ili chama hicho kipate nafasi ya kujiandaa na uchaguzi. Anaripoti Hamis Mguta … (endelea).
Mrema ameiambia MwanaHALISI Online tarehe 23 Agost 2019 alipoulizwa kuhusu muelekeo wa Chadema katika chaguzi za serikali za mitaa na Mkuu wa 2020 na kueleza kuwa hadi sasa tume ya uchaguzi haijatangaza tarehe rasmi ya uchaguzi wa serikali za mitaa wala kanuni na hawajajulishwa maandalizi yamefikia wapi.
“Kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa mpaka sasa serikali haijatoa kanuni labda watoe leo na hatujajulishwa tarehe ya uchaguzi wala hatujui kanuni za mchezo, tunawataka watoe kanuni kwasababu ni haki yetu ili kuweza kujiandaa, hii nchi ni kubwa na ni watu wengi wanakwenda kugombea hivyo bila kupata kanuni mapema hatuwezi kuwafikia tukawapa huo utaratibu,” amesema.
Alipoulizwa kuwa kumekuwa na maelezo ya kuwa chadema wamekuwa watu wa kutoa malalamiko kila wakati na si watu wa kufanya kwa vitendo amesema “Mwenye wajibu wa kutangaza kanuni siyo chadema ni serikali lakini tuhoji kwanini hamtangazi kanuni? tunaonekana tunalalamika, tukihoji kwanini tarehe hazitangazwi mapema tunaonekana tunalalamika, mambo mengine ni mikakati ya ndani lakini niwaondoe hofu watanzania kwamba tunaendelea kujipanga,” amesema.
Kuhusu matukio ya kukamatwa kwa waandishi wa habari kuongezeka pamoja na ugumu wa wanaharakati katika kukosoa mambo mbalimbali Mrema ameiambia MwanaHALISI Online kuwa kinachotokea sasa ndicho walichokuwa wamekipigania kupitia kampeni ya maandamano ya Umoja wa Kupinga Udikteta Tanzania (Ukuta) iliyotangazwa na chama hicho tarehe 1 Septemba, 2016 ambapo walieleza ya kuwa wakimaliza kushughulikiwa wanasiasa rungu litahamia kwa makundi mengine.
“Nakumbuka tarehe 1 Septemba 2016 tulitangaza Ukuta lakini watu hawakutuelewa, hii leo wanapita njia ile ile ambayo tuliwaeleza kwamba wakimaliza na kushughulika na vyama vya siasa watafuata makundi mengine, tuzuie mtu yoyote anayetaka kuharibu nchi yetu na tuunganishe nguvu.
“Bado tunaendelea kuwasemea waliopo magerezani kama akina Erick Kabendera, wengine wamepotea kama kina Azory na Ben Saanane bado tunaendelea kuwatafuta na kuwasemea kwa niaba yao wapo, kuna wengine wameumizwa kama Tundu Lissu bado tupo nao pamoja,” amesema.
Leave a comment