SERIKALI imeombwa iwalipe fidia wafanyabiashara waliopoteza mali zao katika tukio la moto uliounguza sehemu ya Soko Kuu la Kariakoo, jijini Dar es Salaam. Anariopti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumanne, tarehe 13 Julai 2021 na Kaimu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Kanda ya Pwani, Baraka Mwago, akizungumza na wanahabari mkoani Dar es Salaam.
Tukio hilo lilitokea usiku wa Jumamosi, tarehe 10 Julai mwaka huu na kusababisha wafanyabishara zaidi ya 200, kupoteza mali zao kufuatia tukio hilo.
Mwago amesema kuwa, asilimia kubwa ya wafanyabiashara hawatakuwa na fedha za mtaji, hivyo inatakiwa wapatiwe msaada wa kifedha kwa ajili ya kuendelea na biashara zao.
“Wale wenye mikopo tujiulize itachukua muda gani kurudisha mkopo? Wengi tulioongea nao wanasema hawana fedha mali zao zote zimepotea. Hawana fedha taslimu, fedha yao yote walizungushia kuweka kwenye mali iliyopotea,”
https://youtu.be/P0i73cKNS-w
“Serikali inabidi ichukue hatua kupitia kadhia hii, tunawaomba waone namna ya kuwalipa fidia wafanyabaishara wote waliopata majanga ya moto. Kwa jana tulivyoongea nao, soko lina wafanyabiashara wanaojuana wote, hivyo wanajulikana Serikali iwalipe fidia,” amesema Mwago.
Baada ya tukio hilo kutokea, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, aliunda tume ya uchunguzi ili kubaini chanzo chake na athari za moto huo.
Tume hiyo inatarajia kumaliza kazi ya uchunguzi Jumapili, tarehe 18 Julai mwaka huu.
Pia, Waziri Majaliwa aliziomba taasisi za kifedha ziwape muda wa ziada, wafanyabiashara wanaodaiwa, kulipa mikopo yao.
Akizungumzia hatua hiyo, Mwago amesema imeleta faraja kidogo kwa wafanyabiashara hao. “Waziri miuu alitoa neno la faraja aliposema benki zitoe muda ili waliokopa warejesha mikopo yao.”
Leave a comment