CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimeomba huduma ya utoaji chanjo ya ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (Covid-19), iwe ya lazima badala ya hiari kama ilivyotangazwa na Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumatatu, tarehe 19 Julai 2021 na Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, akizungumza na wanahabari jijini Mwanza.
“Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan, iweke utaratibu mzuri wa chanjo kuwa ya lazima kwa Watanzania,” amesema Mbowe.
Aidha, Mbowe ameitaka Serikali iongeze juhudi katika kutoa elimu kwa wananchi juu ya kujikinga na maambukizi ya Covid-19, kwa kuwa wengi hawachukui tahadhari dhidi ya janga hilo.
“Lakini public awareness (uelewa kwa umma) haiko, wala usifikiri Watanzania hawana akili, wamedanganywa hawajui washike la rais au la nani,” amesema Mbowe.

Mbowe ameongeza “ wameweka usugu hawaogopi Corona, wanafikiri ugonjwa huu wanaambukiza wachache.”
Wakati huo huo, Mbowe ameiomba Serikali iweke mkakati wa kutoa matibabu ya Covid-19 bure kwa wananchi, kwa kuwa wengi hawana uwezo wa kumudu gharama za matibabu.
“Kitu kikubwa hatujakijua ni gharama za matibabu, kimsingi gharama za Covid-19 ilipaswa kusimamiwa na Serikali kwa asilimia 100,” amesema Mbowe na kuongeza:
“Sababu janga limetengazwa la kidunia na Shirika la Afya Duniani (WHO). Serikali na nchi zake zinawajibika kuwatibu na kuwakinga wananchi.”
Serikali ya Tanzania, imesema imekamilisha muongozo wa kuingiza na kutoa chanjo ya Covid-19, na kwamba zitaingizwa nchini hivi karibuni.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Prof. Abel Makubi, alisema chanjo hiyo itatolewa bure kwa wananchi watakaohitaji.
Leave a comment