CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimemtaka Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia na Habari, Nape Nnauye aviache vyombo vya habari vitimize wajibu wake kuhusu suala la mikutano ya hadhara ambayo tarehe 21 na 22 Januari mwaka huu chama hicho kitaizindua rasmi katika mikoa ya Mwanza na Mara.
Pia kimemtaka aheshimu kauli ya Rais Samia Suluhu Hassan kwamba wanaCCM wanatakiwa kujibu hoja zinazoibuliwa kwenye mikutano hiyo ya hadhara kwa hoja. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Hayo yamejiri baada ya wiki iliyopita Nape kuviasa vyombo vya habari akiviasa vyombo vya habari kwamba vi-balance taarifa zinazoibuka kwenye mikutano ya hadhara kuhusu serikali.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo tarehe 15 Januari, 2023, Mkurugenzi wa Mambo ya Nje, Itikadi na Uenezi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), John Mrema amesema kauli hiyo ya Nape imetoka wakati si sahihi.
“Nape anataka kuturudisha kwenye usiku wa giza ambapo tunapambana kutoka huko kwenda kwenye mwanga. Kauli hii ni malengo yake ni kuvitisha vyombo vya habari visirushe mikutano mubashara kwa sababu kama unarusha mubashara utapata wapi fursa wa kwenda kubalansi hiyo stori serikalini?
“Nape atuachie, rais samia ameshasema amewambia wanachama wa chama chake wakajibu hoja, nape aviache vyombo vya habari vifanye kazi yake kwa uhuru visirudi kule tulipotoka kwenye zama za giza,” amesema.
Aidha, ameviomba vyombo vya habari visiwe na hofu kwa sababu siku zote wao huzungumza kwa hoja.
“Mikutano yetu inaendeshwa kwa hoja na ajenda mahsusi, tunamtaka waziri wa habari aviache vyombo vya habari vitimize wajibu wake, vyama vya siasa vitimize wajibu wake, ili tuende sasa tukajenge Taifa kwa pamoja kwa mshikamano bila vitisho, bila kurudishana nyuma kwa sababu zama hizo za giza tunapambana kutoka huko kuingiza zama za mwanga,” amesema.
Aidha, amesema maandalizi ya kurejea kwa Makamu Mwenyekiti wa chama hicho bara, Tundu Lissu yanaendelea vizuri na vyombo vya habari vitapewa rasmi taratibu na njia atakayopita.
“Suala la mapokezi yatakuwaje, jukumu hilo litafanywa na uongozi wa kanda ya Pwani mapema iwezekanavyo. Ngazi ya taifa tunaenda Mwanza na Musoma tarehe 21 na 22 hatimaye tutarudisha Dar es Salaam kuja kushirikiana na viongozi wa kanda ya Pwani katika maandalizi na mapokezi ya kiongozi wa chama chetu,” amesema.
Leave a comment