CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimemwomba Rais Samia Suluhu Hassan, aruhusu mikutano ya hadhara kabla ya marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa, ili wanasiasa wapate haki yao ya kikatiba ya kukusanyika na kueleza sera zao kwa wananchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Jumamosi, tarehe 22 Oktoba 2022 na Katibu Mkuu wa Chadema, John Mnyika wakati akizungumza na wanahabari, jijini Dar es Salaam.
“Tunatoa wito kwa Rais na Serikali kujitokeza bila kusubiri marekebisho ya kinachoitwa kanuni za Vyama vya Siasa za mwaka 2019 na marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa Serikali iondoe zuio haramu la mikutano ya hadhara,” amesema Mnyika.
Aidha, Mnyika amemshauri Rais Samia kuanzisha mjadala wa kitaifa kuhusu upatikanaji katiba mpya, kabla ya mchakato huo kufufuliwa.
“Pendekezo la mwisho la kikosi kazi linasema mchakato wa Katiba Mpya uendelee, hata hivyo mjadala wa kitaifa kuhusu Katiba Mpya uanze kabla ya kuanza kwa mchakato wa kuandika Katiba Mpya ili kujadili ajenda muhimu ambazo wamezitaja katika taarifa hiyo,” amesema Mnyika.
Mnyika ametoa wito huo ikiwa ni siku moja tangu Rais Samia akabidhiwe ripoti ya Kikosi Kazi alichokiunda Kwa ajili ya kukusanya maoni juu ya uimarishaji demokrasia ya vyama vingi, kinachoongozwa na Mwenyekiti Profesa Lwekaza Mukandara.
Akizungumza katika mkutano wa kupokea ripoti hiyo, jijini Dar es Salaam, Rais Samia alisema mikutano ya hadhara haitaruhusiwa hadi Sheria ya Vyama vya Siasa na kanuni zake za 2019, itakapofanyiwa marekebisho kwa ajili ya kuondoa vifungu vyenye mapungufu, ikiwemo kinachoipa mamlaka Jeshi la Polisi kuingilia mikutano hiyo.
Kuhusu mchakato wa katiba mpya, Rais Samia alisema Serikali yake inalifanyia kazi huku akieleza kwamba kazi hiyo ni nzito.
Leave a comment