MAKAMU Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Tundu Lissu, anatarajia kurejea nchini kesho tarehe 25 Januari, 2023 saa saba na nusu mchana na kuhutubia wanachama wa chama hicho katika Uwanja wa Buriaga, Temeke jijini Dar es Salaam. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa ya ratiba ya msafara wa Lissu imetolewa leo tarehe 24 Januari 2023 na Mwenyekiti wa Kamati ya Mapokezi ya Lissu ambaye pia Mjumbe wa Kamati ya Chama hicho, Mchungaji Peter Msigwa
Msigwa amesema Lissu atapokelewa na wafuasi na viongozi wa chama hicho kisha msafara wake utaelekea kwenye Uwanja cha Buriaga ambapo kutakuwa na mkutano wa hadhara.
“Lissu ataambatana na viongozi wengine wa chama hicho kwa ajili ya mkutano wa hadhara kwenye kiwanja cha Buriaga Temeke kwa hiyo kama Mwenyekiti nasema maandalizi yote yamekamilika tunawakaribisha wananchi wote wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani” amesema Msigwa.
Lissu atahutubia wanachama wa chama hicho juu ya mambo mbalimbali yanayohusu mwenendo na hali ya siasa nchini.
Msigwa amesema kuwa Lissu ataungana na viongozi wengine kwenye mikatano ya hadhara ambayo Chadema itaifanya nchi nzima.
“Ajenda za mikutano yetu zitakuwa changamoto za vikokoto ugumu wa maisha na mambo kadhaa yanayoendelea kama Mwenyekiti wetu alivyozindua mikutano ya hadhara kule Mwanza”
Kuhusu suala la usalama Lissu Msigwa anasema Serikali imethibitisha hadharani kuwa Lissu na Watanzania wengine waliondoka nchini kwa sababu mbalimbali za kisiasa watakuwa salama.
Wanachama wengine kurudi
Mchungaji Msigwa amesema kuwa Lissu hatorejea peke yake bali atarea na wanasiasa wengine walioondoka nchini wakati hali ya siasa ilipokuwa tete.
Amesema Ezekiel Wenje atarejea nchini wiki hii lakini Godbless Lema Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema ratiba ya kurejea kwake itatangazwa.
Leave a comment