BAADA ya Mahakama Kuu ya Tanzania kuwang’oa wakurugenzi wa halmashauri kusimamia chaguzi, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kimeibuka na madai saba. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
John Mrema, Mkurugenzi wa Uenezi, Itikadi, Mawasiliano na Mambo ya Nje akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika tarehe 13 Mei 2019, ameeleza mambo saba muhimu ili kupatikana kwa chaguzi huru nchini.
Mrema ameeleza madai hayo saba kuwa ni kupatikana kwa Tume Huru ya Uchaguzi, matokeo ya uchaguzi wa rais kupingwa mahakamani, haki ya mgombea kukata rufaa.
Mengine ni mfumo usiruhusu mgombea kupita bila (kupingwa) kupigiwa kura, mfuko Maalum wa Fedha kwa ajili ya kuendesha shughuli za TIEC kusimamia uchaguzi, maamuzi ya Tume Huru ya Uchaguzi kuweza kupingwa mahakamani na kuwepo kwa mgombea binafsi.
“Mapendekezo hayo ni kwa ajili ya maslahi ya nchi hasa Watanzania wanapojiandaa kuelekea kwenye chaguzi mbili muhimu, Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (2019) na Uchaguzi Mkuu (Rais, Wabunge na Madiwani-2020).
“… ambapo wapiga kura wanahitaji kuhakikishiwa kuwa, karatasi za kura sio tu ziko salama, bali hazitaangaliwa kama karatasi zingine za kawaida,” amesema Mrema.
Amesema kuwa, kuundwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi (TIEC) ambayo itawekewa utaratibu mpya wa uteuzi kuwapata wajumbe wake.
“Mathalani katika nchi za Kenya, Afrika Kusini, Malawi au Ghana, watu hao wanapatikana kwa kutuma maombi ya kazi na kufanyiwa vetting (uchambuzi) na mamlaka husika kabla ya uteuzi.
“Uteuzi uwe huru, usiwe chini ya mtu mmoja ambaye naye anakuwa na maslahi binafsi au ya chama chake wakati wa uchaguzi. Tunataka wajumbe wa tume wawe na uhakika wa usalama wanapotimiza majukumu yao. Muhula wao kazini ujulikane na ulindwe. Masharti yao ya kazi yajulikane,” amesema.
Hata hivyo amesema, hakuna haja ya kuendelea kuwepo na zuio la kutoruhusu maamuzi ya Tume ya Uchaguzi kuhojiwa mahakamani.
“Lakini pia kama tume ni huru, kunakuwa na hofu gani ya kuzuia maamuzi yake kuhojiwa mahakamani? Maana yake basi hiyo tume isiyohojiwa mahakamani haiko huru,” amesema.
Hata hivyo, amepongeza uamuzi wa Mahakam Kuu ya Tanzania kufuta vifungu 7(1) na 7(3), vya Sheria ya Taifa ya Uchaguzi namba 5 ya mwaka 1985, vilivyokuwa vikiwapatia mamlaka wakurugenzi wa halmashauri nchini kusimamia uchaguzi.
Leave a comment