KAMATI Kuu ya Chadema imeazimia kususia chaguzi ndogo zinazotarajiwa kufanyika hivi karibuni kutokana na kutoridhishwa na uendeshwaji wa chaguzi ndogo zilizopita. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Akizungumza kuhusu maazimio ya kamati hiyo iliyoketi jana tarehe 18 Septemba 2018 jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe amedai kuwa kumekuwa na hujuma katika chaguzi ndogo ikiwemo wakurugenzi kutumika katika kuhakikisha wagombea wa CCM wanapita bila kupingwa.
Mbowe amesema kamati hiyo imefikia uamuzi wa kutoshiriki chaguzi ndogo hasa uchaguzi unaotarajiwa kufanyika kwenye jimbo la Liwale na kata 37, baada ya kutafakari yaliyotokea kwenye chaguzi ndogo za ubunge za Ukonga, Monduli na kata 23 Jumapili iliyopita ya Septemba 16, 2018.
“Kwa sasa tunakwenda kufanya mabadiliko ndani ya chama, tunakwenda kujijenga na hatuwezi kushiriki wakati tunaonewa na sheria hazifuatwi. Kwa sasa tunarudi nyuma,” amesema.
Mbowe ametaja baadhi ya matukio aliyodai kwamba yamebaka demokrasia, pamoja na wasimamizi wa uchaguzi ambao ni wakurugenzi kufunga milango pindi wagombea wa Chadema wanaporudisha fomu pamoja na wasimamizi wa vituo vya kupigia kura kutotambulika mapema huku suala hilo likifanyika kwa makusudi maalumu.
Matukio mengine aliyotaja Mbowe ni baadhi ya viongozi wa umma kufanya kampeni kinyume na sheria na baadhi ya wasimamizi wa uchaguzi katika vituo vya wapiga kura ambapo mawakala walizuiliwa kuingia kutumika kupiga kura.
Leave a comment