CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeeleza maendeleo ya afya ya mwanachama wake Mdude Nyagali, amejeruhiwa kichwani. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Kwa sasa, Mdude amelazwa kwenye Hospitali ya Rufaa Mbeya akipatiwa matibabu ya majeraha aliyopata, baada ya kutekwa na kuteswa na watu wasijojulikana.
Akizungumza na Wanahabari leo tarehe 9 Mei 2019 jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje, John Mrema amesema, majira ya asubuhi Mdude aliingizwa katika chumba cha upasuaji kwa ajili ya kufanyiwa upasuaji.
Mrema amesema, Mdude aliyepatikana jana tarehe 8 Mei 2019 baada ya kuachwa na watu wasiojulikana, amefanyiwa vipimo mbalimbali ikiwemo cha CT Scan na kubainika kwamba, amepata matatizo maeneo ya kichwani.
“Madaktari wananedelea na vipimo na uchunguzi wa afya yake katika Hospitali ya Rufaa ya Mbeya asubuhi ameingizwa chumba cha upasuaji baada ya vipimo vya CT Scan kwenye kichwa.
“Madaktari wamempeleka moja kwa moja kwenye chumba cha upasuaji, labda watatoa taraifa za kitaalamu hapo baadaye,” amesema Mrema.
Amesema, kabla ya Mdude kupelekwa katika chumba cha upasuaji, alihojiwa na maafisa wa polisi kuhusu tukio la kutekwa kwake na watu wasiojulikana.
“Tangu leo asubuhi saa 12.00 polisi wa vyeo mbalimbali walikwenda hospitalini na kutaka kumhoji pamoja na kwamba ufahamu wake haukurudi vizuri na walitaka taarifa ili waweze kukamata watekaji, wa kwanza ni RPC na RCO wa Mbeya,” amesema Mrema na kuongeza.
“Baada ya dakika chache alifika OCD wa Mbeya Mjini na wao walichofanya walifanya mahojiano lakini baada ya muda saa tatu asubuhi RCO wa mkoa wa Songwe akiongozana na timu ya wapelelezi, walifika hospitalini wakamhoji na kuchukua maelezo yake pamoja kwamba, anaongea kwa tabu walichukua wanayokumbuka,”amesema.
Leave a comment