MADIWANI wa vyama viwili, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na wale Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wamezichapa wakati wa uchaguzi wa Naibu Meya wa Manispaa ya Ilala, Jijini Dar es Salaam leo tarehe 3 Oktoba 2018. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Chadema ndio waliokuwa wakija juu zaidi baada ya kuwatuhumu CCM kuiba kura za upinzani kwenye uchaguzi huo uliofanyika katika Ukumbi wa Anatoglou ambapo Diwani wa Kata ya Vingunguti, Omar Kumbilamoto (CCM) ametangazwa kushinda.
Omar ambaye awali alikuwa kwenye nafasi hiyo kupitia Chama cha Wananchi (CUF) na baadaye kuhamia CCM na kisha kusimamishwa kugombea udiwani kwenye uchaguzi mdogo wa marudio uliofanyika hivi karibuni, alitangazwa mshindi wa unaibu meya wa Ilala kwa kupata kura 27 ambapo Adam Rajabu (CUF) alipata kura 25 huku mwakilishi wa Chadema Patrick Assenga akitoka kapa (0).
Kitimtimu kilianza pale uchaguzi ulipomalizika na kura kubebwa kisha kupelekwa kwenye chumba cha kuhesabia kura, Patrick (Chadema) alianza kupiga yowe akituhumu mikakati ya CCM aliyodai kuanza kuvuruga uchaguzi kwa kuiba kura.
Patrick alipiga kelele akidai Rajab alikuwa amebeba kura zake ambazo zilikuwa 27 ambapo polisi walimvaa na kumwamuru arudishe kura hizo na kwamba, matokeo yakapinduliwa kwa kura za CUF zikapelekwa CCM na zile za CCM zikadaiwa kuwa ndio za CUF.
Wakala wa Kumbilamoto alitoka akishangilia kwamba, mgombea wake (Omar) ameibuka mshindi kwenye uchaguzi huo. Kitendo hicho kiliwaghadhibisha madiwani wa upinzani na hapo ulianza ugomvi kwa kupigana ngumi kati ya madiwani wa Chadema, CUF na wale wa CCM huku matusi yakiwatoka madiwani wa upinzani. Hali hiyo ilisababisha polisi kuingilia kati na kutuliza ghasia.
Leave a comment