CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema Bajeti inayopendekezwa na serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 ina mapungufu makubwa yanayotishia hata utekelezaji wake, anaandika Pendo Omary.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Dk. Vincent Mashinji, Katibu Mkuu wa Chadema amesema chama hicho kinaendelea na uchambuzi wa bajeti hiyo kabla ya vikao vya Bunge la Bajeti kuanza mwishoni mwa mwezi huu.
Dk. Mashinji ametolea mfano wa bajeti inayopendekezwa katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi akisema; “Jeshi la Zimamoto na Uokoaji katika fungu la 14 – wametengewa Sh. 11,187,079,115 (bilioni 11) kwa ajili ya miradi matumizi mengineyo lakini fedha kwa ajili ya miradi ya maendeleo ni Sh. 1.5 bilioni ambazo zitanunua magari 2 ya zimamoto.
“Fedha za uendeshaji zimetengwa Sh. 3 bilioni tu, kwahiyo tujiandae pale majanga ya moto yakitokea kwani hakuna fedha za kununua dawa za kuzimia moto zilizotengwa.”
Dk. Mashinji pia ameeleza kusikitishwa na fungu lililotengwa kwaajili ya Jeshi la Magereza. Katika fungu hilo la 28, Sh. 5 bilioni kwa ajili ya kuendesha shuguli zote za magereza nchini, ilihali sare za askari pekee ziliombewa na Sh. 4.198 bilioni hata hivyo wamepewa Sh. 25 milioni tu.
“Vifaa vya wafugwa kama magodoro, shuka, sufuria za kupikia waliomba Sh. 1.692 bilioni lakini wamepewa Sh. 50 milioni, sare za wafungwa ziliombewa Sh. 1.980 bilioni lakini wamepewa Sh. 20 milioni tu.
“Mafunzo kwa ajili ya askari wapya ziliombwa Sh. 4.650 bilioni lakini hawajapewa fedha hivyo hakutakuwa na askari wapya wala waliopo kupanda vyeo,” amesema Dk. Mashinji.
Amesema kuwa gharama za kuhamia Dodoma waliomba Sh. 1.2 bilioni lakini hakuna fedha zilizotegwa. Chakula cha wafungwa zilitakiwa Sh. 48.223 bilioni lakini zimetegwa Sh. 18.615 bilioni kwa wafungwa na mahabusu 36,000 waliopo. Maana yake kwa siku mfugwa au mahabusu atakula chakula kwa Sh. 1,436 tu.
“Tunawasihi wabunge wote waungane bila kujali vyama vyao kuisimamia na kuiwajibisha serikali kwa mujibu wa Katiba na kuhakikisha kuwa Bunge haliwi chombo cha kupitisha mapendekezo ya serikali, kuanzia kwenye Kamati za Bunge,” amesisitiza Dk. Mashinji.
Leave a comment