Tuesday , 23 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa CCM yawaweka kikaangano mawaziri sita
Habari za Siasa

CCM yawaweka kikaangano mawaziri sita

Spread the love

 

KATIBU Mkuu wa chama tawala nchini Tanzania- Chama Cha Mapinduzi (CCM), Daniel Chongolo amesema, chama hicho kitaita mawaziri sita ili kujiridhisha juu ya mipango yao katika kutatua kero za wananchi kutokana na upungufu walioubaini kwenye ziara zake na Sekretarieti. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).

Aidha, Chongolo amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Joseph Mkirikiti kuunda kikosikazi cha kukagua na kufanya tathmini ya miradi inayotekelezwa mkoani kwake, ili kujua kama utekelezaji wake unakidhi thamani ya fedha zilizotumika na kutoa huduma kusudiwa kwa wananchi.

Katibu Mkuu huyo alisema hayo akiwa katika ziara ya kikazi mkoani humo ambapo aliweka bayana, kuwa hawajaridhishwa na utekelezaji wa miradi mingi inayotekelezwa.

Akizungumza katika kikao cha majumuisho, Chongolo aliwaambiwa wajumbe wa kikao hicho, yeye na Sekretarieti yake wakifika Dodoma, watawaita Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk Dorothy Gwajima, Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, Waziri Kilimo Profesa Adolf Mkenda na Waziri wa Ardhi, William Lukuvi.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi

Wengine ambao Sekretarieti inatarajia kuwaita ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Ummy Mwalimu na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro.

“Tutakaporejea Dodoma tutawaita mawaziri wanaohusika na sekta za afya, maji, ardhi, kilimo, TAMISEMI na maliasili na utalii ili kujiridhisha, juu ya mipango yao na kujua wamejipangaje kutatua kero za wananchi zenye kufanana na walizobaini mkoani humo,” alisema Chongolo.

Alisema katika ziara hiyo, kuna mambo mengi ambayo yanahitaji majibu kwa viongozi hao wateule wa Rais hivyo wanawajibu kujibu mbele yao kwa kuwa CCM ndicho chama tawala.

Dk. Dorothy Gwajima, Waziri wa Afya wa Tanzania

Chongolo alisema wao kama Sekretarieti ya chama ambacho Ilani yake inatekelezwa kwa miaka mitano, watahakikisha wanafuatilia utekelezaji wa maagizo na maelekezo, ambayo yapo kwenye Ilani ili kutatua changamoto za wananchi hasa vijiji.

Aidha, Katibu huyo alitumia kikao hicho kumwagiza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mkirikiti kuunda kikosi kazi cha kukagua na kufanya tathmini ya miradi inayotekelezwa mkoani hapo.

“Namemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Rukwa kuunda kikosi kazi cha kukagua na kufanya tathmini ya miradi inayotekelezwa mkoani kwake ili kujua kama utekelezaji wake unakidhi thamani ya fedha zilizotumika na kutoa huduma ilivyokusudiwa kwa wananchi,” alisema.

“Hatukuridhishwa na miradi tuliyotembelea, hasa katika sekta ya afya ambayo inakabiliwa na changamoto kubwa, ya upungufu mkubwa wa dawa, wataalamu, huduma duni kwa wazee na maeneo mengine kuwa na utekelezaji wa miradi isiyoendana na thamani ya fedha iliyotumika,” alisema Chongolo.

Juma Aweso, Waziri wa Maji

“Naagiza na kukuelekeza Mkuu wa Mkoa, uunde timu ya wataalamu ya kukagua na kufanya tathmini ya miradi yote inayotekelezwa mkoani kwako, ili kujua hali halisi ya kinachoendelea hususan kwenye eneo la thamani ya fedha zilizotumika hapa, mambo hayaendi vizuri kabisa,” aliongeza.

Chongolo alisema CCM haiko tayari kulea viongozi na watendaji wazembe wanaoonekana kushindwa kutatua kero za wananchi, na kuimarisha ustawi wao, hivyo kati siku 14 atahitaji ripoti ya utekelezaji wa maelekezo hayo na hatua kali zichukuliwe itakapobainika kuna ubadhirifu au uzembe.

“Nahimiza watendaji wa Serikali kuwa waadilifu kwa kuheshimu fedha za umma. Hakikisheni fedha zinazoletwa au kutengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo, zinatafsirika kwa wananchi kwa kuwaletea unafuu na kuimarisha huduma za kijamii na kiuchumi kwao,” alisema.

“Ni lazima tuogope fedha za umma, ukizitumia vizuri zitakujengea heshima, ukizitumia vibaya zitakuvunjia heshima kwa wananchi, hivyo kila mmoja anapaswa kuwa mwadilifu katika kusimamia dhamana aliyopewa,” alisema Chongolo.

 

Katibu Mkuu alisema kila kiongozi na mtendaji katika chama na Serikali, anatakiwa kutimiza wajibu wake kwa kuhakikisha upatikanaji wa tija kwenye huduma za kijamii unakuwepo, kama ilivyosisitizwa kwenye Ilani ya Uchaguzi na anavyosisitiza Rais Samia Suluhu Hassan wakati wote.

Chongolo na Sekretarieti yake, wako katika ziara ya kujitambulisha na kukagua miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali ambapo jana walikuwa Songwe, baada ya kutoka Rukwa.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Rais Samia aridhishwa utendaji mabalozi, awapa neno

Spread the loveRais wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan amewapongeza mabalozi  wanaowakilisha ...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

NMB yadhamini Mkutano Mkuu ALAT, kufunguliwa na Samia

Spread the loveBENKI ya NMB, imekabidhi hundi yenye thamani ya Sh. 120...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mipango na uwekezaji kutumia bilioni 121.3, mradi wa Bagamoyo wapewa kipaumbele

Spread the loveWIZARA ya Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji, imeliomba Bunge...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mbunge ataka kasi uzalishaji walimu ipunguzwe akidai hakuna ajira

Spread the loveMBUNGE wa Mlalo (CCM), Rashid Shangazi, ameishauri Serikali ipunguze kasi...

error: Content is protected !!