CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimemteua Sheha Mpemba Faki, kuwa mgombea wake katika uchaguzi mdogo wa Konde, visiwani Zanzibar, unaotarajiwa kufanyika tarehe 18 Julai 2021. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma…(endelea).
Akizungumza na wanahabari leo tarehe 22 Juni 2021, jijini Dodoma, Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM, Shaka Hamdu Shaka, amesema Faki ameteuliwa kugombea nafasi hiyo na Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya chama hicho (NEC).
“Kama mnavyofahamu kuna uchaguzi mdogo katika Jimbo la Konde, mkoani Kaskazini Pemba, tunategemea utafanyika Julai. Upande wa Kamati Kuu imefanya uteuzi wa Faki, atakayesimama katika nafasi ya ubunge wa jimbo hilo,” amesema Shaka.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), iliitisha uchaguzi huo mdogo kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa Konde (ACT-Wazalendo), Khatib Said Haji, kilichotokea tarehe 20 Mei 2021, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, alikokuwa anapatiwa matibabu.
Mwili wa Khatib ulizikwa nyumbani kwao Pemba visiwani Zanzibar, siku hiyo hiyo aliyofariki dunia.
Leave a comment