MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, amebaini Wakala wa Ndege za Serikali (TGFA), ililipa Sh.3.92 bilioni kugharamia matengenezo ya ndege ambayo ilikuwa haifanyi kazi tangu mwaka 2015. Anaripoti Matrida Peter…(endelea).
Kichere amebainisha hayo kwenye ripoti zake za ukaguzi wa mwaka 2019/20, ambazo leo Alhamisi tarehe 8 Aprili 2021, ameiwasilisha bungeni jijini Dodoma.
“Nilibaini kuwa, TGFA ililipa jumla ya Sh. bilioni 3.92 mnamo tarehe 14 Februari na 26 Aprili 2018 ikiwa ni gharama za huduma ya matengenezo makubwa ya ndege aina ya Fokker 28-5H-CCM ya mwaka 1978.”
Charles Kichere, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)
“Hata hivyo, wakati wa ziara yangu kwenye hifadhi ya ndege za Serikali Dar es Salaam mnamo 19 Agosti 2020, nilibaini kuwa ndege hiyo ilikuwa haifanyi kazi na ilikuwa imetelekezwa tangu mwaka 2015,” amesema Kichere
“Aidha, niligundua kuwa, TGFA iliwasilisha suala hili Wizara ya Fedha na Mipango ikiomba ifanyike tathmini ya kina juu ya ndege hiyo ili kuweza kuishauri Serikali juu ya uamuzi sahihi wa hatua za kuchukua.”
Kichere amesema, “hata hivyo, ninaona uamuzi wa kuwekeza fedha za walipa kodi zenye thamani ya Sh.3.92 bilioni kufanya ukarabati mkubwa wa ndege bila kufanya tathmini ya kina ya gharama na faida haukuwa sahihi, na hivyo, kusababisha hasara kwa taifa.”
More Stories
Mama mzazi wa IGP Sirro afariki dunia
CAG: Nyaraka za kughushi zilitumika Jeshi la Zimamoto
CAG: Taasisi 10 zimepata hati mbaya, 81 zenye shaka