SERIKALI imeshauriwa kumruhusu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Assad kufanya ukaguzi maalum kwenye miradi ya maji kutokana na uwepo wa madai ya miradi hiyo kutekelezwa chini ya kiwango. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Ombi hilo limetolewa leo tarehe 16 Novemba 2018 bungeni jijini Dodoma, na Mbunge Viti Maalum, Conchesta Rwamlaza akisema kwamba kuna malalamiko mengi ya miradi ya maji kutekelezwa chini ya kiwango, na kushauri CAG kufanya ukaguzi maalum ili kujua utekelezwaji wa miradi hiyo na kiasi cha fedha kilichotumika katika utekelezwaji wake.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Maji, Juma Aweso amesema haina haja ya kuagiza ukaguzi maalum wa CAG kwa kuwa wizara imeunda timu maalum ya wataalam kwa ajili ya kukagua miradi ya maji hasa maeneo ya vijijini.
“CAG amekuwa akifanya ukaguzi kila mwaka, ukaguzi wa miradi kuhusu ufanisi na utaalamu hufanyika kila mwaka, CAG ameshafanya ukaguzi kwenye usimamizi wa uchimbaji wa visima vya maji na miradi iliyokamilkia, taarifa ya ukaguzi ilikaguliwa na kuwasilishwa bungeni, ukaguzi wa ufanisi na wa kitaalamu , serikali haina haja ya kuagiza ukaguzi maalum, wizara iliunda timu ya wataalam maalum kukagua miradi ya maji vijijini,”amesema Aweso.
Leave a comment