KIASI cha Sh 18.5 bilioni zilizokusanywa na Kampuni ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KADCO) kama malipo ya tozo za kutumia uwanja wa ndege na abiria, hazikupelekwa Mamlaka ya Mapato. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Hayo yamebainishwa leo Jumanne tarehe 12 Aprili 2022 na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, wakati akizungumza na waandishi wa Habari jijini Dodoma.
Amesema Kampuni ya KADCO inakusanya tozo za kuondoka kwa abiria kutoka kwa waendeshaji wa mashirika ya ndege lakini haipeleki kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato kama inavyotakiwa na sheria.
“Kuanzia Julai 2019 hadi Juni 2021 KADCO ilikusanya Sh. bilioni 2.37 na dola za Marekani milioni 7.04 (sawa na Sh. bilioni 16.13) kama tozo za kuondoka kwa abiria lakini hazikuwasilishwa kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato kinyume na sheria,”
Kutokana na hali hiyo Kichere ameitaka KADCO izingatie matakwa ya sheria na kuwasilisha kwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania makusanyo ya tozo za kuondoka kwa abiria katika viwanja vya ndege.
Leave a comment