SIKU moja baada ya Bunge la Jamhuri kuazimia kutofanya kazi na Profesa Mussa Assad, Mthibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), mkaguzi huyo ametoa tahadhari. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Mdhibiti huyo amesema, Bunge linapaswa kuangalia athari ya kile wanachokiamua kwa mapana yake na kwamba, taasisi hiyo (Bunge) ilipaswa kutafuta suluhu ya kile kilichotokea.
Prof. Assad ametoa kauli hiyo leo tarehe 3 Aprili 2019 wakati akizungumza na Televisheni ya Taifa (TBC). jana, Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge ilimtia hatiani kwa kudaiwa kulidhalilisha Bunge kwa kusema ni dhaifu.
Aidha amesema, Bunge limechukua umechukuliwa pasina na kutathimini athari zake huku akisisitiza kwamba, walipaswa kufanya tathmini ya kina nini kitatokea baada ya uamuzi huo.
“Mi nafikiri tukae chini tutazame, halafu tuone athari ni zipi ili kuepuka matatizo ambayo tunaweza kuyasababisha .Wasiwasi wangu ni kuwa, huenda likaja kuwa tatizo kubwa zaidi badala ya kupata suluhisho, “ amesema Prof. Assad.
Hata hivyo, Prof. Assad ameiomba Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kuweka wazi hansadi ya maswali na majibu kuhusu mahojiano yake, yaliyotokana na kosa lililokuwa linamkabili la kulidhalilisha Bunge.
Amesema, ni vyema hansadi ya kamati hiyo ikawekwa wazi kwa kila mtu, ili Watanzania wajue alichohojiwa na majibu yake, na kwamba kwa kufanya hivyo, Watanzania wanaweza kupima kama uamuzi wa Bunge wa kumtenga ni sahihi ama si la!.
“Rai yangu ile hansadi ya Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge iwekwe wazi kwa kila mtu ili kila mtu ajue nimeulizwa kitu gani na nimejibu kitu gani, ili kila Mtanzania aweze kuweka tathimini yake halafu aweze kupima kuwa hili lilipofikiwa ni sawa au sio sawa,” amesema Prof. Assad.
Mapema jana Mwenyekiti wa Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, Emmanuel Mwakasaka aliwasilisha bungeni ripoti ya mahojiano baada ya Prof. Assad kufika mbele ya kamati yake kujibu tuhuma za kudharau Bunge.
Tuhuma hizo ziliibuliwa na Job Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri mwaka jana kwamba, Prof. Assad alilidhalilisha Bunge wakati alipofanya mahojiano na Kituo cha Redio ya Umoja wa Mataifa.
Wakati akiwasilisha ripoti hiyo, Mwakasaka alisema, uchunguzi pamoja na mahojiano aliyofanyiwa Prof. Assad, umemtia hatiani kwa kuwa, kauli yake ilikiuka Sheria na Kanuni za Bunge huku (Prof. Assad) akisisitiza kuendelea kutumia neno hilo – dhaifu – kwa kuwa ni la kawaida katika lugha za kikaguzi
Leave a comment