MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Charles Kichere, ameonyesha wasiwasi kwa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), kupata hasara ya Sh.3.39 bilioni kutokana na usimamizi usioridhisha. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam … (endelea).
Kichere amebainisha hilo, kwenye ripoti yake ya ukaguzi kwa mwaka 2019/20 ambayo tayari imekwisha wasilishwa bungeni jijini Dodoma.
Amesema, tarehe 21 Aprili 2011, NIDA iliingia mkataba na M/s IRIS Corporation Berhad ya Malaysia (Supplier) kwa ununuzi wa bidhaa na vifaa vya utekelezaji wa mfumo wa kadi za taifa kwa kutumia teknolojia ya kisasa.
Mfumo huo, ulikuwa wa gharama ya Dola 149,956,303. Muda wa mkataba uliisha tokea tarehe 14 Machi 2018 (miaka mitatu nyuma) bila ya kuongezwa kwa muda.
Kichere amesema, “ukaguzi wangu wa mkataba huu, umebaini kulikuwa na makubaliano ya kusambaza kadi milioni 25 mpaka kipindi cha ukaguzi, Novemba 2020, nilibaini msambazaji aliwasilisha kadi milioni 13.73 tu.”
“Aidha, uchambuzi wangu ulibaini, kati ya kadi zilizowasilishwa, NIDA imetumia kadi milioni 6.18 kutengeneza vitambulisho vya taifa na kubakiza kadi milioni 5.08 zikiwa hazijatumika,” amesema
Kichere amesema, “hata hivyo, nimebaini kati ya kadi milioni 5.08 zilizobakia, ni kadi milioni 4.65 tu, ndizo zilikuwa zimehifadhiwa kwenye bohari, huku kadi 426,757 zenye thamani ya Sh.3.39 bilioni zikiwa zimeharibika na hazifai kwenye matumizi ya kutengeneza vitambulisho vya taifa.”
Amesema, licha ya menejimenti ya NIDA kueleza kuwa imetuma barua kwenda kwa mkandarasi (IRIS) ili afanye usuluhisho wa kadi zilizoonekana na matatizo na kubadilisha na kadi mpya “ni maoni yangu kuwa kuna hatari ya NIDA kupata hasara ikiwa IRIS atashindwa kubadilisha kadi hizo ambazo hazifai kutokana na kukosekana kwa mkataba halali kati ya NIDA na M/s IRIS Corporation Berhad.”
Leave a comment