SELEMAN Bungara maarufu ‘Bwege,’ Mgombea Ubunge Kilwa Kusini kupitia ACT-Wazalendo, amesema, kama Watanzania watamchagua tena Dk. John Magufuli kuwa Rais wa Tanzania katika Uchaguzi Mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020, wasilalamike kuhusu ugumu wa maisha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Magufuli ni Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) anasaka nafasi ya kukamilisha vipindi viwili vya uongozi, tangu alipoingia madarakani tarehe 5 Novemba 2015.
Bwege ameyasema hayo leo Jumamosi tarehe 26 Septemba 2020 katika uzinduzi wa kampeni za mgombea ubunge wa Ubungo kupitia chama hicho, Renatus Pamba katika viwanja vya Mabibo jijini Dar es Salaam.
“Kama Watanzania mnakubali wakati wa Rais Magufuli maisha ni magumu na wakati wa Rais Jakaya Kikwete (2005-2015) kulikuwa na afadhali mliikataa CCM, nitawashangaa sana mkimchagua Magufuli mtajipiga wenyewe msilie,” amesema Bwege.
Huku akishangiliwa na umati wa wananchi kwenye mkutano huo, Bwege amesema katika uchaguzi wa mwaka huu, Rais Magufuli hatoshinda kwa maelezo kwamba katika uongozi wake wananchi wengi hawakuwa na maisha bora.
“Nawauliza Watanzania wakati wa Rais Magufuli na Rais Jakaya Kikwete bora wapi kimaisha,” aliulizana kujibiwa “Kikweteeeeeee”
Kisha Bwege akasema “Wa CCM wanakubali bora wakati wa Kikwete na wapinzani wanakubali bora wakati wa Kikwete. Ikiwa kwa Kikwete mambo yalikuwa afadhali na sasa mabaya kwa nini Magufuli ashinde?”
Wakati huo huo, Bwege amewaomba wananchi wa Ubungo wamchague Pamba kwa kuwa ni kiongozi bora atakayetatua shida zao.
“Wananchi wa Ubungo, mchagueni Pamba na madiwani wote wa ACT-Wazalendo ili mpate mabadiliko,” amesema Bwege.
Leave a comment