TAASISI ya Mwalimu Nyerere imesema, Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 ukiwa wa amani, huru na haki utawezesha kupatikana viongozi bora. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea)
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo, Joseph Butiku wakati akitoa salamu za taasisi kwa wajumbe wa mkutano mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) unaofanyika ukumbi wa Mlimani City Dar es Salaam.
“Nawashukuru kwa mwaliko wa kunikaribisha mimi kwa niaba ya Taasisi ya Mwalimu Nyerere.”
“Nimekuja kuwaona mlivyo, mmependeza. Mwenyekiti (Freeman Mbowe) unapendeza,” amesema Butiku huku akishangiliwa na wajumbe wa mkutano mkuu
Amesema, Taifa letu linadumu katika amani, Taifa letu linapata maendeleo ya watu kutokana na juhudi zao wenyewe kwa njia za kujitegemea.
“Taifa letu lina miaka 59. Utaratibu huu wa vyama vingi ni miaka 28. Tulipata uhuru ili tujitawale, ili tujisimamie mambo yetu wenyewe na utaratibu wa vyama vingi ulianzishwa ili kuboresha utawala bora na kuendesha nchi kujumuisha wananchi wote.”
“Tumedumu katika utamaduni huo kwa changamoto zilizokuwepo. Sisi kwenye taasisi siyo wanasiasa ila tunapenda kushauri, ili tupate viongozi wote tuzingatie sheria inayolinda mambo haya na taratibu zote,” amesema Butiku.
Mwenyekiti huyo amesema “bahati mbaya, tunayumba kidogo lakini uchaguzi wa mwaka huu utaonyesha uhuru, wazi na wa haki.”
“Uchaguzi ukiwa hivyo, utatupatia viongozi bora na viongozi hao walinde msingi wa Taifa letu wanadumu katika usawa na Taifa linadumu katika haki kwa wote,” amesema
Akihitimisha salamu zake, Butiku amesema “nawatakieni mkutano mwema. Rafiki yangu (Tundu) Lissu tulikutana zamani tulipokuwa tunazungumza mambo ya nchi” naona uko imara. Kauli hiyo ilimfanya Lissu aliyekuwa kando yake kutabasamu huku wajumbe wakishangilia
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment