WAKATI Kamati ya Bunge ya Bajeti ikiishauri Serikali kupunguza kukopa katika soko la ndani ili kuipa nafasi sekta binafsi kukopa, yenyewe imeongeza kiasi inachotarajia kukopa mwaka ujao wa fedha ikilinganishwa na kiasi ilichokopa mwaka huu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Katika mwaka wa fedha 2021/22 Serikali ilikusudia kukopa jumla ya Sh4.99 trilioni na hadi kufikia mwezi Aprili 2022 mikopo kutoka vyanzo vya ndani ilifikia Sh. 4.12 trilioni sawa na asilimia 82.57 ya lengo.
Kutokana na hali hiyo kamati leo Alhamisi tarehe 16 Juni, 2022, imeishauri Serikali kupunguza kukopa ndani “ili kuipa nafasi sekta binafsi kupata mikopo kwa riba nafuu ili kuchochea uwekezaji na hatimaye kukuza uchumi wa nchi.”
Mbali na ushauri huo wa Kamati, Serikali imeongeza zaidi makadirio ya kukopa katika soko la ndani kutoka Sh 4.99 mwaka 2021/22 hadi Sh 5.78 trilioni mwaka 2022/23.
Kati ya kiasi kinachotarajiwa kukopwa na Serikali Sh3.30 trilioni ni kwa ajili ya kulipia hatifungani na dhamana za Serikali zinazoiva na kiasi cha Sh2.48 trilioni ni kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo.
Leave a comment