KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, imeshauri Mabaraza ya Kata yaunganishwe kwenye mfumo wa mahakama, ili kudhibiti mianya ya rushwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Ushauri huo umetolewa leo Jumatatu tarehe 28 Aprili 2021, na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Sillo Daniel Baran wakati akiwasilisha maoni ya kamati hiyo kuhusu utekelezaji wa Bajeti ya Mfuko wa Mahakama kwa mwaka wa fedha 2020/21.
Kamati hiyo imetoa ushauri huo ikidai, kumekuwa na udhaifu wa kiutendaji katika kutoa haki na kutatua migogoro.
“Serikali iangalie suala la Mabaraza ya Kata kuunganishwa kwenye Mfumo wa Mahakama kwani kumekuwa na udhaifu wa kiutendaji katika kutoa haki na kutatua migogoro,” imeshauri kamati hiyo.
Kamati hiyo imesema “mabaraza ya usuluhishi yalianzishwa kwa Sheria namba 5 Sura 216, kwa nia njema ya kusaidia utoaji haki katika maeneo ambayo hayajafikiwa na mahakama.
“…lakini mabaraza haya badala yake yamekuwa yakiongoza katika kuwanyima wananchi haki kutokana na baadhi yake kutawala kwa rushwa na kushughulikia kesi ambazo hawana mamlaka ya kisheria ya kuzishughulikia.”
Kamati hiyo ya Bunge ya Bajeti imeeleza, asilimia kubwa ya watu wanaounda mabaradha hayo, hawana uelewa wa sheria.
“Aidha, mabaraza haya yanasimamiwa na kamati ya maendeleo ya kata, miongoni mwa kanuni za baraza ni baraza kuundwa na wananchi wa kawaida tu wasio na uelewa wa sheria suala ambalo linapelekea haki kutotolewa kwa usawa.
“Hivyo, Kamati inashauri Mabaraza haya kuunganishwa kwenye Mfumo wa Mahakama na hivyo kuruhusu utoaji haki ikiwa ni pamoja na ukataji rufaa Mahakama ya Mwanzo pindi itakapobidi,” imesema taarifa hiyo na kuongeza.
Na kwamba, maboresho haya pia yafanyike pia kwa mabaraza mengine yanayotumika kutoa haki mathalani Mabaraza ya Ardhi ili kuleta haki na usawa kwa wananchi.
Leave a comment