BUNGE limeitaka serikali iwachukulie hatua za kisheria wote waliotajwa katika ubadhilifu wa posho ya resheni (posho ya chakula) ya jumla ya Sh 888.5 milioni kwa watumishi wasio askari. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akiwasilisha bungeni taarifa ya shughuli za Kamati ya Hesabu za Serikali kwa mwaka 2018 Mwenyekiti wa Kamati hiyo leo tarehe 1 Februari 2019, Nagwenja Kaboyoka amesema, kufuatia vigezo na mambo ya msingi katika uchambuzi wa taarifa ya CAG, uimebainisha kwamba, kulifanyika malipo ya pesa hizo kama posho.
Amesema, malipo hayo yalilipwa kwa watumishi ambao siyo askari kinyume na taratibu za Jeshi la Polisi.
Amesema kuwa, Ofisa Masuhuli alifahamisha kamati kuwa hatua za kinidhamu zimechukuliwa kwa kuwasimamisha kazi watumishi wanne wanaotuhumia kufanya malipo hayo
Aliwataja watumishi hao kuwa ni Frank Msaki aliyekuwa Mhasibu Mkuu,Ida Moyo aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha mishahara,Damian Bupamba aliyekuwa Mhasibu kitengo cha mishahara na Inspekta Mwita Mirambo.
Alisema Ofisa Masuuli alifafanua kwamba watu wengine watatu wasio watumishi wa serikali walioshirikiana na watumishi hao wamekamatwa na kupewa dhamana wakati taratibu za kiupelelezi zikiendelea.
Aliwataja watu hao kuwa ni Ibrahim Mlilima,Nassoro Mlilima na Lodrick Massawe.
Na kwamba, hoja ya kamati katika hili ni pamoja na kugundulika kwa ubadhirifu mkubwa wa fedha za umma tangu mwaka 2016 hadi 2019 na kwamba, watuhumiwa bado hawajafikishwa mahakamani ili kujibu tuhuma zinazowakabili.
Amesema, uchunguzi wa jambo hilo umechukua muda mrefu kukamilika hivyo kuwepo kwa uwezekano wa fedha za umma kupotea bila hatua stahiki kuchukuliwa kwa wahusika.
Mwenyekiti huyo amesema, Bunge linaazimia kwamba serikali iwachukulie hatua kali na za kisheria wahusika waliohusika katika ubadhilifu huo ndani ya kipindi cha miezi miwili.
“Na kutoa taarifa kwa Bunge kuhusu utekelezaji wa azimio hili,”amesema Kaboyoka.
Leave a comment