MBUNGE wa Singida Mashariki, Tundu Lissu amekuja juu baada ya Bunge la Jamhuri kufuta mshahara na posho zake zote. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Lissu ametoa taarifa hiyo jana tarehe 13 Machi 2019 kupitia waraka aliousambaza akidai kuwa, bunge limezuia mshahara wake na posho za kibunge tangu mwezi Januari mwaka huu.
Katika taarifa yake hiyo, Lissu anasema sababu ya kuzuiliwa kwa mshahara na posho zake ni kutokuwepo kwake bungeni .
“Leo napenda kuthibitisha kwamba uamuzi wa bunge kunifutia mshahara na posho zangu ulifanyika kabla hata ya Spika Ndugai kuombwa na kutoa mwongozo huo. Ndiyo kusema kwamba bunge la Spika, Job Ndugai na Katibu wa Bunge, Stephen Kagaigai limezuia mshahara na posho za bunge tangu mwezi Januari mwaka huu,” ianeleza sehemu ya taarifa Lissu.
Lissu amesema hatua hiyo ya Bunge ni ukiukaji wa katiba na sheria na kueleza kuwa, mshahara na posho za kibunge hutolewa kwa mbunge iwe amehudhuria vikao au hajahudhuria vikao.
“Iwe itakavyokuwa, uamuzi wa kunifutia mshahara na posho za kibunge ambazo kila mbunge hulipwa awe anaumwa au mzima awe amehudhuria vikao bunge au hajahudhuria. Ni uthibitisho mwingine wa utamaduni wa ukiukaji wa katiba, sheria na taratibu ambazo umekithiri.
“Aidha kitendo hicho ni uthibitisho mwingine wa chuki kubwa ambayo imetamalaki dhidi yangu binafsi na dhidi ya wale wote tuliokataa kumsujudia Magufuli na watu wake.” inaeleza sehemu ya taarifa ya Lissu.
Lissu yuko nje ya nchi tangu mwezi Septemba mwaka 2017 baada ya kushambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana mjini Dodoma. Miongoni mwa sababu anazotoa Lissu kuhusu kutorejea kwake nchini hadi sasa ni matibabu.Baada ya kukumbwa na tukio hilo, Lissu alitibiwa katika hospitali zilizoko nchini Kenya na Ubelgiji.
Leave a comment