KAMATI ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, leo tarehe 31 Agosti, 2021, imemtia hatiani Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima (CCM) kwa makosa ya kudhalilisha, kuchonganisha Bunge na mihimili mingine, Serikali na wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Akiwasilisha taarifa ya kamati hiyo kuhusu uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa zinamkabili Gwajima, Mwenyekiti wa kamati hiyo, Emmanuel Mwakasaka amesema kamati imependekeza vyombo vya kisheria vifuatilie mienendo ya Askofu Gwajima.
Alisema kwa kuwa Askofu Gwajima alikiri kauli zote zilizolalamikiwa kuwa ni za kwake, Kamati imependekeza Bunge liazimie kumpa adhabu ya kutohudhuria mikutano miwili ya Bunge.
“Kuna viashiria vya uwepo wa jinai na uvunjifu wa amani. Pia suala hili lishughulikiwe kwa mujibu wa kanuni na maadili ya viongozi wa umma sambamba na chama chake CCM kimchukulie hatua,” alisema Mwakasaka.
Alisema licha ya Gwajima kutakiwa kutoa ushahidi wa tuhuma alizozitoa, hakuwa na vielelezo vyovyote vya kuhusu kauli alizozitoa ikiwamo kutuhumu viongozi wa serikali kupewa hela ili kuruhusu chanjo iletwe nchini.
Leave a comment