KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), limeiagiza Serikali isimamie mapato na matumizi ya halmashauri nchini, ili kudhibiti upotevu wa fedha za umma. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Kamati hiyo ilitoa agizo hilo juzi tarehe 17 Februari, 2022 bungeni jijini Dodoma kuhusu uchambuzi wa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa, kwa mwaka wa fedha ulioishia tarehe 30 Juni 2020.
Ni baada ya uchambuzi wa LAAC, kubaini mapungufu katika mifumo ya ukusanyaji mapato na matumizi ya halmashauri.
Taarifa hiyo ya LAAC, iliyotolewa na Mwenyekiti wake, Grace Tendega, imedai kuna ujanja unaofanyika katika mifumo ya kielektroniki ya kukusanya na kutunza kumbukumbu za mapato, kitendo kinachoathri nia ya Serikali kuongeza ufanisi katika zoezi hilo.
Kufuatia dosari hizo, LAAC imeishauri Serikali iimarishe usalama na udhibiti wa miamala katika mfumo wa mapato (LGRCIS), ikidiwa kuna mianya inayoruhusu ubadhirifu kwa njia ya mtandao katika mashine za kukusanyia mapato (POS).
Agizo hilo lilitolewa na LAAC, baada ya uchambuzi wake juu ya ukaguzi wa CAG kwa mwaka wa fedha wa 2020, kubaini kuna miamala ya fedha kiasi cha Sh. 4.5 bilioni, ilifutwa baadhi ya halmashauri kinyume na utaratibu.
“CAG amebaini na kamati imethibitisha kuwa, katika baadhi ya halmashauri, miamala ya makusanyo hufutwa au hurekebishwa, bila ya kuwapo kwa uthibitisho kwamba ilikosewa. Katika mwaka wa Fedha 2019/20, jumla ya Sh. 4.5 bilioni, zilifutwa kwenye mfumo kwa utaratibu hu ambao Kamati haikubali,’ ilisema taarifa ya LAAC.
Taarifa hiyo imetaja halmashauri zilizohusika katika ufutwaji wa miamala hiyo bila uthibitisho, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Siha (Sh. 624.2 milioni), Tunduru (Sh. 1.2 bilioni), Nanyumbu (Sh. 497 milioni), Kilindi (Sh. 320 milioni) na Liwale (Sh. 258 milioni).
Pia, LAAC iliitaka Serikali ipige marufuku vitendo vya baadhi ya halmashauri kukusanya fedha za mapato kisha kuzituma bila ya kuzipeleka benki, ambvyo vinasbabaisha fedha hizo kutobainika katika mifumo ya kielektroniki ya mapato (LGRCIS) na matumizi (EPICOR/MUSE).
“Kwa mujibu wa taarifa ya CAG , jumla ya Shilingi 18.769 bilioni zilizokusanywa katika halmashauri mbalimbali, zilitumika kabla ya kupelekwa benki katika mwaka wa fedha 2019/20,” ilisema taarifa ya LAAC.
Kamati hiyo ya Bunge, ilitaja Halmashauri za Wilaya zilizoguswa na hoja hiyo, ambazo ni Kaliua (Sh. 183.2 milioni), Uyui (Sh. 383.4 milioni), Siha (Sh. 112.5 milioni), Itilima (Sh. 54.9 milioni), Chalinze (Sh. 25.2 milioni) na Manispaa ya Temeke (Sh. 344 milioni).
Ripoti ya 2020. Je wahusika walichukuliwa hatua za kisheria? Kila mwaka tunarudia hadithi hii ya Alfu Leila. Hakuna kinachofanyika