WAKALA wa Usajili wa Biashara na Leseni nchini (BRELA), imetangaza kusudio la kufanya operesheni endelevu ya kuzifuta kampuni zinazokiuka sheria, ambapo zaidi ya 5,000 zinatarajiwa kufutwa katika awamu ya kwanza, endapo wamiliki wake hawatathibitisha. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kusudio hilo limetangazwa leo Ijumaa, tarehe 27 Mei 2022 na Afisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
Nyaisa amesema, kampuni zitakazofutwa ni zile zilizokiuka Sheria ya Makampuni, ikiwemo kwa kutowasilisha taarifa za mwaka, kushindwa kutimiza malengo kusudiwa ya uanzishwaji wake pamoja na kuelemewa na migogoro baina ya wamiliki.
“Natangaza kusudio la kufuta kampuni 5,676, kama sehemu ya awamu ya kwanza ambayo tunahisi hayafanyi biashara kwa kutimiza matakwa ya kisheria kama nilivuyeleza hapa juu,” amesema Nyaisa.
Mtendaji huyo wa BRELA amesema, wakala unafuta usajili wa kampuni hizo ili ubaki na kampuni zilizo hai, kupunguza majina ya kampuni yasiyofanya kazi na kuzuia kutumika na watu wengine na kupunguza vishoka wanaouza majina hayo.
Aidha, Nyaisa amesema BRELA itatoa notisi ya awamu tatu kwa ajili ya wamiliki kupata fursa ua kuthibitisha iwapo kampuni zao zinafanya kazi.
Leave a comment