BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imebaini kuongezeka kwa udanganyifu wa fedha nchini unaohusisha mwananchi kupokea taarifa(hati au barua pepe) inayodai kuwa ni uthibitisho wa malipo kupitia SWIFT au mifumo mingine ya uhamishaji fedha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa ya BoT kwa umma iliyotolewa leo Ijumaa ikielezea utapeli huo unavyofanyika imesema kuwa mpokeaji anafahamishwa kuwa fedha zimeingizwa kwenye benki au akaunti katika taasisi ya fedha nchini Tanzania.
“Wakati mwingine, mpokeaji fedha anaelekezwa kulipa kiasi fulani cha fedha kuwezesha kupata fedha hizo nyingi,” imesema taarifa hiyo.
BoT imesema matukio mengi ya taarifa hizo yanahusisha kiasi kikubwa cha pesa kinachodaiwa kuletwa kwa ajili ya ufadhili wa mradi au matumizi binafsi.
“Hivyo, Benki Kuu ya Tanzania inapenda kuutaarifu umma kwamba taarifa hizo ni za kughushi na za kubuni,” imesema taarifa hiyo.
Aidha wananchi wameshauriwa kuwa waangalifu na kuacha kujihusisha na miamala hiyo ambayo kwa kawaida inalenga kuwatapeli fedha.
Pia, wananchi wamekumbushwa kuzingatia kanuni bora za kufanya miamala ya fedha ili kuepuka upotevu wa fedha ambazo ni ikiwemo kuhakikisha usalama wa taarifa za fedha wakati wa kutoa taarifa binafsi mtandaoni (tovuti, mitandao ya kijamii), kupitia barua pepe au kwenye simu.
Wameshauriwa kutojihusisha kujibu barua pepe, barua au simu zinazoahidi kupokea fedha kutoka kwa watu au kampuni wasizozifahamu vizuri na kuwa waangalifu mnapofanya malipo ya mtandaoni kwa kufanya uhakiki wa mshirika wa kibiashara (mtu au kampuni) kabla ya kutoa maelezo au kufanya malipo.
Aidha, wananchi waliokumbwa na matatizo hayo wameshauriwa kutoa taarifa kwenye vyombo vya usalama kwa hatua stahiki.
Leave a comment