KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) nchini Tanzania, Daniel Chongolo amesema, hakuna Taifa ulimwenguni limeendelea pasina kukopa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Chongolo amesema hayo leo Jumanne, tarehe 4 Januari 2022, Ikulu jijini Dar es Salaam, katika hafla ya Rais Samia Suluhu Hassan kupokea taarifa ya utekelezaji wa matumizi ya Sh.1.3 trilioni za maendeleo kwa ustawi wa taifa dhidi ya UVIKO-19.
Fedha hizo ni mkopo usiokuwa na riba kutoka Shirika la Fedha Duniani (IMF). Fedha hizo zimeelekezwa kwenye sekta ya maji, elimu, afya na miundombinu.
Akizungumza katika hafla hiyo, Chongolo amesema, watu wote wanapiga kelele ya mikopo na mambo mengine, lakini wananchi wana uhakika wa watoto wao kuingia darasani pindi shule zitakapofunguliwa.
Amesema, kwa zaidi ya miaka 30, kumekuwa na tatizo madarasa na kusababisha kuwapo na machaguo ya wanafunzi hadi mara tatu, lakini ukimwona mpinzani wako anakusifia jiulize kuna nini na ukimwona anapigia kelele jambo hilo, endelea nalo.
“…wapo watu wengi wanasema unajua kukopa na maneno mengi, katika dunia ya sasa, mtu yoyote aliyeendelea bila kukopa natamani siku moja anyooshe mikono,” amesema Chongolo
Bosi huyo wa CCM amesisitiza, “lakini duniani hakuna taifa lisilokopa na ukiangalia mataifa yanayoendelea, yanaongoza kukopa kuliko sisi.”
Chongolo amezungumzia suala hilo la mikopo ikiwa ni takribani wiki moja imepita tangu Spika wa Bunge, Job Ndugai alipokosoa uataribu wa serikali kuendelea kukopa kugharamikia miradi ya maendeleo.
Spika Ndugai alisema, ikiwa madeni yakiwa makubwa yanaweza kusababisha nchi ikapigwa mnada.
Kauli hiyo ya Spika Ndugai iliibua mjadala ikiwamo kwa viongozi wa mikoa wa CCM kumshambulia kwa kauli hiyo kwamba ina lengo la kumwamisha Rais Samia.
Jana Jumatatu, Spika Ndugai alijitokeza mbele ya waandishi wa habari akimwomba radhi Rais Samian na wananchi kwa kauli yake kwamba hakuwa na lengo la kumpinga Rais Samia.
Leave a comment