MBUNGE wa Viti Maalumu, Sophia Mwakagenda ameitaka Serikali kuvunja bodi ya chai ya Wilaya ya Rungwe kwa sababu wananchi hawana imani na bodi hiyo na haina faida kwao, anaandika Dany Tibason.
Mwakagenda alitoa kauli hiyo wakati akiuliza swali la nyongeza ambao ameema wawekezaji wameingizwa kwenye bodi hiyo ambao kimsingi wanajiwekea matakwa yao.
“Mfano mmiliki wa WATCO (Kiwanda cha Wakulima Tea Company) ni mwekezaji kutoka nje wakati Mohamed Enterprise ni mzawa na serikali imemwambia aombe kibali upya, Je serikali iko tayari kuvunja bodi hii,” alihoji.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, William Ole Nasha amesema bei ya chai hupangwa kwa mkutano wa wadau na kanuni inaruhusu majadiliano kufanyika kati ya mkulima na mnunuzi.
Kuhusu kuvunjwa kwa bodi, Ole Nasha amesema katika hali kama hiyo ni vigumu kusema moja kwa moja bodi ivunjwe lakini akaahidi kuambatana na mbunge huyo kuwatembelea wakulima hao.
Awali, katika swali lake la msingi Mwakagenda alihoji ni kwanini wakulima wa chai Wilaya ya Rungwe wanalazimishwa kuuza majani mabichi ya chai kwa bei ndogo kuliko wakulima wa chai wa Wilaya ya Njombe na Lushoto.
Ole Nasha amesema bei dira ya majani mabichi ya chai hupangwa katika mkutano mkuu wa wadau wa chai ambao ni wa kisheria na hufanyika kila mwaka kabla ya msimu kuanza.
Amesema kwa kuwa bei dira hupangwa na kukubaliwa na wadau wote, tofauti ya bei kati ya eneo moja na jingine hutokana na majadiliano kati ya wakulima na wenye viwanda kama ilivyoainishwa kwenye kanuni.
“Kwa upande wa Rungwe bei ni kati ya Sh 240 na 250 ambayo ni juu ya bei ekelezi. Tofauti ya bei kwa maeneo hayo inatokana na malipo ya pili. Kwa mfano katika mwaka 2015/16, Kampuni ya Uniliver inayomiliki viwanda vya Kibwele, Kilima na Lugoda imelipa malipo ya pili kati ya Sh 80 hadi 200 kwa kilo.
Leave a comment