KUELEKEA mchezo wa kesho Jumamosi dhidi ya Yanga, Nahodha wa klabu ya Simba, John Bocco amesema wamejipanga vizuri kwa ajili ya mchezo huo, huku akikiri mchezo huo utakuwa mgumu kuibuka na ushindi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo utachezwa kesho majira ya saa 11 jioni kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam huku klabu ya Yanga ikiwa mwenyeji.
Nahodha huyo amesema licha ya kupata muda wa kujiandaa kuelekea mchezo huo, ambao utakuwa mgumu kutokana na wapinzani wao Yanga kuwa na mchezo mzuri kwa sasa katika ligi hiyo.
“Sisi kama wachezaji tumejiandaa vizuri na tumepata maandalizi mazuri na tunakwenda kucheza mchezo mgumu, kwani ukiangalia hata wao wametuzidi pointi ila tutapambana na ninaamini Mungu atatusaidia,” amesema Bocco ambaye ana magoli manne.
Timu hizo zimecheza michezo tisa kila moja, Yanga ikiwa na pointi 23 katika nafasi ya pili huku Simba ikiwa nafasi ya tatu ikiwa na pointi 19, wakati vinara wa ligi hiyo Azam FC wakiwa na pointi 25 baada ya kucheza michezo 10.
Yanga inaingia katika mchezo huo ikiwa na kumbukumbu ya kutoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Gwambina, huku watani wao Simba wanawavaa wapinzani wao wakitoka katika ushindi wa bao 2-0 walipichaka Kagera Sugar.
Nahodha huyo anakwenda kuongoza safu ya mashambulizi ya Simba ambao mpaka sasa wamefunga jumla ya mabao 21 kwenye michezo tisa waliocheza, huku Yanga wakiwa wamefunga mabao 11.
Leave a comment