KUFUATIA klabu ya Simba kutangazwa kuwa mabingwa wapya wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2020/21, washambuliaji Prince Dube wa Azam FC, John Bocco, Chris Mugalu na Meddie Kagere kutoka Simba wameingia kwenye Ligi mpya ya kusaka kiatu cha ufungaji bora huku ikisalia michezo miwili. Anaripoti Kelvin Mwaipungu…(endelea)
Bao la dakika 13, la John Bocco kwenye mchezo dhidi ya Coastal Union kutoka Tanga, lilimfanya kuwa kinara kwenye msimamo wa wafungaji kwenye michezo ya Ligi Kuu Bara mara baada ya kufika mabao 15.
Nafasi ya pili kwenye orodha hiyo ya wapachikaji mabao inashikwa na mshambuliaji Prince Dube, Raia wa Zimbabwe anayekipiga kwenye klabu ya Azam Fc akiwa na mabao 14, ukiwa ni msimu wake wa kwanza ndani ya Ligi Kuu Bara.
Kwa upande wa Chris Mugalu juzi kwenye mchezo dhidi ya Coastal Union, aliandika bao lake la 13 kwa msimu huu na bao la pili kwenye mchezo huo, ambao Simba walitangaza ubingwa kwa mara nne mfululizo.
Nafasi ya nne kwenye upachikaji mabao inashikwa na mfungaji bora wa Ligi hiyo kwa misimu miwili Meddie Kagere ambaye mpaka sasa ameweka kambani mabao 11, licha ya kutopata nafasi ya kuanza mara kwa mara kwenye kikosi cha kwanza toka ujio wa kocha Didier Gomes, mwezi Januari, mwaka huu.
Washambuliaji hao wote kwa sasa wamebakisha michezo miwili, kabla ya kumaliza kwa msimu huu ambao upo ukingoni.
Huwenda Bocco na Prince Dube wakapewa nafasi kubwa ya kutwaa kiatu hiko, kutokana na kupata nafasi ya kuanza kwenuye kikosi cha kwanza, kwenye klabu zao, tofauti na Mugalu na Kagere.
Katika kinyang’anyiro hiko, Dube na Mugalu ndio msimu wao wa kwanza kwenye Ligi kuu toka wasajiliwe kwenye klabu zao na kuonekana kufanya vizuri.
Leave a comment