KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa Tanzania, Salum Mayanga amemuongeza kwenye kikosi straika wa Simba, John Bocco kuchukua nafasi ya Mbaraka Yussuf aliyekuwa majeruhi, anaandika Catherine Kayombo.
Bocco ameshafika Afrika Kusini kujiunga na wenzake ambao wanatarajiwa kesho kushuka uwanjani kucheza mchezo wao wa Nusu Fainali ya michuano ya Baraza la Vyama vya Michezo Kusini mwa Afrika (Cosafa) dhidi ya Zambia.
Mshambuliaji huyo anachukua nafasi ya Mbaraka ambaye alipata majeruhi katika moja ya michezo yao ya awali ya kundi A, ambapo walikuwa pamoja na timu za Malawi, Mauritius na Angola.
Mayanga amesema amemuongeza Bocco katika kikosi hicho kwa malengo mawili, moja ni kujaza nafasi hiyo, lakini pia kuongeza nguvu kujiandaa na mchezo wao dhidi ya Rwanda wa kuwania kufuzu fainali za Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wanaochezea ligi za ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Kenya.
Mchezo huo unatarajiwa kufanyika Julai 15, mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza na marudiano yatafanyika mwishoni mwa mwezi au mwanzoni mwa Agosti.
Leave a comment