ROBERT Kyagulanyi (Bobi Wine) ambaye nimpinzani wa Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni, amekamatwa na Jeshi la Polisi katika Kituo cha Kasangati, nchini humo. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Taarifa ya kukamatwa kwa Bobi Wine imetolewa kwenye ukurasa wake wa Twitter, ambapo msimamizi wa ukurasa huo ‘admin’ amesema, mwanasiasa huyo amekamatwa mapema leo tarehe 6 Januari 2020.
Na kwamba, amekamatwa wakati akijiandaa kuhutubia kwenye mkutano wake wa kwanza wa kuhamasisha uungwaji mkono, katika mkakati wake wa kugombea Urais wa Uganda, kwenye uchaguzi wa mwaka 2021.
Mwanasiasa huyo alikamatwa akiwa wilayani Wakiso nchini Uganda, huku wafuasi wake wakisambaratishwa kwa kutumia mabomu ya machozi.
Kwa mujibu wa Jeshi la Polisi nchini Uganda, mkutano wa Bobi Wine ulisambaratishwa, kwa sababu ya eneo uliopangwa kufanyika, kutokuwa na huduma ya choo yenye uwezo wa kukidhi mahitaji ya wafuasi waliofika kushiriki mkutano huo. Lakini sababu hiyo ilipingwa na wafuasi wa Bobi Wine.
Msimamizi wa ukurasa wa Twitter wa Bobi Wine, amesema Jeshi la Polisi limesambaratisha mkutano huo, licha ya kwamba mhusika alikidhi matakwa yote ya kisheria.
Bobi Wine alipanga kufanya mikutano hiyo kwa muda wa siku saba, kuanzia Jumatatu ya leo hadi Jumapili ya tarehe 12 Januari mwaka huu.
Bobi Wine alipanga kufanya mikutano katika Wilaya za Gulu, Wakiso, Lira, Adjumani, Yumbe, Arua na Zombo, nchini Uganda.
Leave a comment