ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana ya Chama cha Wananchi (JUVICUF), Hamidu Bobali, amejiunga na ACT-Wazalendo na kupokelewa na Katibu Mkuu wa chama hicho, Ado Shaibu,.Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Huku aliyekuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya ACT-Wazalendo, kisha kuhamia NCCR-Mageuzi, Juma Nkumbi, akirejea CUF na kupokewa na Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba.
Wanasiasa hao wamechukua hatua hiyo leo Jumamosi, tarehe 5 Februari 2022, jijini Dar es Salaam.
Bobali amesema ameamua kujiunga na ACT-Wazalendo, akidai CUF kimekufa.
“Kama ni kuilea CUF, mimi nimeilea sana. Kama ni kuivuta nimeivuta sana kwa bahati mbaya CUF imejifia kwa kifo kikubwa sana. Nimevumilia mno wakati mwingine nilikuwa nafuatilia kwamba huenda kuna nusu ya haki , lakini haipo na haitopatikana tena,” amesema Bobali.
Bobali amesema “sababu dhamira iliyokuwepo ndani ya CUF sio kupigania haki, bali kugawana rasilimali. Ndiyo jambo liliopo.”
“Naenda nyumbani na kitakachotokea mtasikia, nawathibitishia hakuna CUF nchini. Nawathibitishia Lindi na Mtwara CUF inaenda kumalizika kabisa, sababu tuna hoja na naenda kueleza hawana dhamira ya kujenga chama, bali ya kugawana mbao na mimi nisingependa kuwa miongoini mwa watakaoshuhudia hilo,” amesema Bobali.
Akizungumza baada ya kumpokea Bobali, Ado amesema tukio hilo linashiria uzinduzi wa operesheni ya pili ya shusha tanga, pandisha. Iliyoasisiwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad, ya kushawishi wanachama wa CUF kujiunga na chama hicho.
“Leo kinazindua rasmi operesheni shusha tanga, pandisha tanga awamu ya pili kutokana na mamia ya wafuasi wa vyama pinzani na tawala, walioataka kuingia. Kwa niaba ya chama tunazindua rasmi mchakato wa kupokea vigogo, waliozungumza nasi na kutuomba kujiunga na chama hiki,” amesema Ado.
Katibu Mkuu huyo wa ACT-Wazalendo amesema, orodha ya watu watakaojiunga na ACT-Wazalendo kupitia operesheni hiyo ni ndefu.
“Bobali katika Bunge lililopita alikiuwa ni Mbunge wa Jimbo la Mchinga, sababu bado damu inachemka nadhani sisi vijana safu yetu ilivyo. 2025 tutakuwa naye bungeni kupitia ACT-Wazalendo,” amesema Ado.
Kwa upande wake Nkumbi, amemhakikishia Prof. Lipumba kuwa anakwenda kukisambaratisha ACT-Wazalendo.
“Prof. Lipumba nakuahidi ACT-Wazalendo inasambaratika na nakuahidi hii wiki yote ni mchaka mchaka, kuanzia Jumatatu shughuli inakuwa nzito, tunataka tuwaonyeshe kwamba siasa si ujanja ujanja. Siasa uheshimu watu wanaojenga chama,” amesema Nkumbi na kuongeza:
“Tunarudi nyumbani kuirudisha CUF ambayo ikisimama CCM (Chama Cha Mapinduzi) inatikisika. Huu ni mwanzo mimi nimeambiwa wewe ndenda kama chambo wanaokuja ni mziki mzito.
Mbali na Nkumbi, wanachama wengine zaiudi ya 30 wa ACT-Wazalendo walirejea CUF, akiwemo aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho Mkoa wa Dar es Salam, Sudi Mohamed. Siamini Juma (aliyekuwa Mwenyekiti wa Ngome ya Vijana Jimbo la Mbagala).
Mkurugenzi wa Habari, Uenezi, Mahusiano na Umma CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa, amesema “Mwenyekiti wetu, Prof. Lipumba atawapokea rasmi wageni wetu katika kile tulichokiita awmau ya kwanza kupokea ndugu zetu wanaorudi kwao.”
Leave a comment